Tuesday, April 16, 2013

MAOMBI YA LWAKATARE KUFUTIWA KESI YAZUA TAFRANI MAHAKAMANI, WAANDISHI WA HABARI WAFUNGIWA NJE.

Katika taarifa iliyokutwa katika mtandao wa kijamii wa CHADEMA ilikuwa hivi:-

"Uamuzi wa kusikiliza maombi hayo katika ofisi badala ya mahakama ya wazi ulizua manung’uniko na malalamiko kutoka kwa waandishi, wanachama wa Chadema na wafuasi wao, huku baadhi ya wafuasi wa Chadema wakiwaporomoshea matusi makali Polisi waliokuwa wakilinda usalama mahakamani hapo.


Hata hivyo, Machi 20, 2013, Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), aliwafutia mashtaka, lakini muda mfupi baadaye walikamatwa na kufunguliwa mashtaka hayohayo katika kesi namba 6 ya 2013.
Mawakili wanaomtetea Lwakatare hawakukubaliana na uamuzi huo, hivyo waliwasilisha maombi Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, wakiupinga. Pia waliiomba mahakama hiyo itengue uamuzi huo.
Maombi hayo yalisikilizwa jana na Jaji Lawrence Kaduri, lakini waandishi wa habari walizuiwa kuingia ofisini kwa Jaji Kaduri ambamo kesi hiyo ilifanyika.
Wanahabari walikuwa miongoni mwa watu waliofika mapema mahakamani hapo na kuungana na umati mkubwa wa wanachama na wafuasi wa Chadema kusubiri ukumbi wa mahakama ufunguliwe.
Baadaye walitangaziwa kuwa maombi hayo yatasikilizwa ofisini kwa Jaji Kaduri, hivyo askari Magereza waliwazuia waandishi wa habari kwa maelezo kuwa ofisi hiyo ni ndogo na kwamba tayari ilikuwa imejaa, hivyo hapakuwa na nafasi ya kuingiza watu zaidi.
Miongoni mwa waliopata nafasi ya kuingia katika ofisi ya Jaji Kaduri ni Lwakatare na Ludovick, mawakili wao watatu, mawakili wa Serikali watatu, mke wa Lwakatare na Karani wa Jaji Kaduri.
Wengine ni Mwenyekitiwa Chadema, Freeman Mbowe, Katibu Mkuu, Dk Willibrod Slaa na baadhi ya askari Magereza.Waandishi wa habari walipinga kitendo hicho na baada ya mvutano uliodumu dakika kadhaa, askari hao walimruhusu mwandishi mmoja tu kuwakilisha wanzake.

Kwa kawaida kesi za jinai na hasa zenye mvuto kwa umma kama ilivyo ya Lwakatare husikilizwa katika mahakama ya wazi na hata mawakili walikuwa wamejiandaa kusikiliza maombi hayo katika mahakama ya wazi, kwani walikuwa wamebeba majoho ambayo kwa kawaida huvaliwa kwenye mahakama za wazi.
Uamuzi wa kusikiliza maombi hayo katika ofisi badala ya mahakama ya wazi ulizua manung’uniko na malalamiko kutoka kwa waandishi, wanachama wa Chadema na wafuasi wao, huku baadhi ya wafuasi wa Chadema wakiwaporomoshea matusi makali Polisi waliokuwa wakilinda usalama mahakamani hapo.
Maombi yasikilizwa
Wakili wa Serikali Mkuu, Prudence Rweyongeza akisaidiana na wenzake Peter Maugo na Ponsiano Lukosi alisema DPP alifuta mashtaka ya Lwakatare na mwenzake kwani kesi ya awali ilifunguliwa katika masjala isiyostahili.
Rweyongeza alidai kuwa kesi ya kwanza ilisajiliwa katika kitabu cha kesi zinazosikilizwa na Mahakama za chini, badala ya kitabu cha kesi zinazosikilizwa na Mahakama Kuu.
Aliitaja sababu nyingine kuwa, mahakama ilikosea kwa kuwaruhusu washtakiwa kujibu mashtaka ambayo husikilizwa na Mahakama Kuu pekee.
Katika hoja zao, wadai wakiongozwa na Wakili Peter Kibatala, walisema DPP alikosea kuchukua uamuzi huo kwa kuwa madaraka yake yana mpaka na kwamba hapakuwa na sababu wala mazingira yanayoelezwa katika sheria ya DPP kuchukua uamuzi huo.
Pia Wakili Kibatala akisaidiana na Wakili Tundu Lisu walihoji uhalali wa mashtaka hayo ya ugaidi wakidai kuwa hakuna maelezo yanayoonyesha kuwa mashtaka yanayomkabili Lwakatare na mwenzake ni ya ugaidi. Hivyo waliiomba Mahakama Kuu iyatupilie mbali mashtaka hayo.
Hata hivyo, Rweyongeza alidai ni mapema kutoa hoja za uhalali wa mashtaka kwa kuwa kesi hiyo bado iko katika hatua ya uchunguzi na kwamba baada ya uchunguzi inaweza kuwa na mabadiliko yoyote.
Hatima ya maombi hayo imebaki mikononi mwa Jaji Kaduri ambaye baada ya kusikiliza hoja za pande zote aliahirisha shauri hilo hadi atakapotoa uamuzi wake kwa tarehe ambayo atawajulisha wahusika wa kesi hiyo."

No comments:

Post a Comment

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...