Sunday, April 21, 2013

BOSTON YATULIA BAADA YA MSAKO MKUBWA

Wananchi wa Bosto wakionesha furaha yao baada ya msako kukamilika
 Jiji la Boston linarejea katika hali ya kawaida baada ya mojawapo wa msako mkubwa katika historia ya polisi ya Marekani kumalizika kwa kukamatwa kijana mmoja anayeshukiwa kuhusika katika shambulio la mabomu wakati wa mbio za marathon siku ya Jumatatu.
Shughuli zilisimama katika jiji zima mnamo siku ya Ijumaa wakati polisi waliposambazwa kila pembe kumtafuta mshukiwa huyo Dzhokhar Tsarnaev, mwenye umri wa miaka19.
Alipatikana amejificha bustanini mwa nyumba moja katika kitongoji kimoja na alikamatwa baada ya mapambano ya risasi ambapo alijeruhiwa.
Kaka yake , Tamerlan, aliuwawa awali katika mapambano ya risasi na polisi. .
Watu watatu waliuwawa na zaidi ya 170 walijeruhiwa katika mashambulio ya mabomu ya siku ya Jumaatatu na afisa mmoja wa polisi aliuwawa wakati wa msako wa washukiwa..
Dzhokhar Tsarnaev anazuiliwa chini ya ulinzi mkali hospitali ambako pia wanatibiwa wengi wa waliojeruhiwa na mabomu siku ya Jumatatu.
Maafisa wa polisi wanasema wananuia kumhoji bila ya kumsomea haki zake kama mshukiwa --kama haki yake ya kumwita wakili na kutosema chochote kwa sababu za usalama kwa raia.
Uamuzi huo ulishutumiwa na Jumuiya inayotetea haki za raia nchini Marekani ilioyosema kwamba hatua kama hiyo inahusu tu kesi ambazo zinahusika na vitisho vya papo hapo kwa usalama na wala hakuna sababu ya kumnyima mshukiwa haki hizo.
Lakini baadhi ya wabunge wa chama cha Republican wamehoji kwamba Tsarnaev achukuliwe kama ni-mpiganaji adui ikimaanisha hastahili kupewa haki kama anazopewa mshukiwa wa jinai.

CHANZO:BBC

No comments:

Post a Comment

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...