Wednesday, May 8, 2013

HOTUBA YA MSEMAJI MKUU KAMBI RASMI YA UPINZANI BUNGENI DR.ANTONY GERVAS MBASSA.

HOTUBA YA MHESHIMIWA DR ANTONY GERVAS MBASSA (MB) MSEMAJI MKUU WA KAMBI RASMI YA UPINZANI WIZARA YA AFYA NA USTAWI WA JAMII KUHUSU MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI KWA MWAKA WA FEDHA 2013/2014 (Inatolewa kwa mujibu wa Kanuni za Kudumu za Bunge kanuni ya 99(9) toleo la mwaka 2013).


 1.0 RASILIMALI WATU KATIKA SEKTA YA AFYA
Mheshimiwa Spika, hatuwezi kuongelea au kuzungumzia hali ya sekta afya nchini bila ya kuangalia mambo makuu mawili yanayoifanya sekta hiyo kuonekana na kuiwezesha kuwa na tija. Mambo hayo makuu kwanza ni rasilimali watu katika sekta hiyo na pili madawa na vifaa vya kutolea tiba. Wizara ya afya na ustawi wa jamii ilianzisha mpango mkakati wa rasilimali watu wa mwaka 2008-2013 unaoitwa 'Human Resources Strategic Plan' unaolenga kutoa muongozo jinsi gani ya kupanga na kupambana na tatizo la rasilimali watu katika sekta ya afya lakini mpaka hivi sasa tatizo la rasilimali watu limekuwa likiongezeka kwa kasi ya ajabu na halijapatiwa ufumbuzi wa kutosha.
Mheshimiwa Spika, taarifa iliyotolewa na McKinsey & Company  mwaka 2006 kufuatia  tafiti  uliofanywa  na McKinsey & Company’s Global Public Health practice, hasa kufuatia taarifa yao waliyoito hapo mwaka 2003  inayoitwa, “ Acting Now to Overcome Tanzania’s Greatest Health Challenge: Addressing the Gap in Human Resources for HealthMapungufu ya  rasilimali watu katika sekta ya afya inaonyesha kuwa Tanzania ina upungufu mkubwa wa raislimali watu, na pia hakuna mfumo au kanuni maalum inayotumiwa na Wizara katika kugawanya  rasilimali watu chache iliyopo katika mikoa na wilaya mbali mbali hapa nchini. Jambo hili limepelekea wilaya nyingi hapa nchini kukosa kabisa  madaktari katika hospitali za wilaya.
Mheshimiwa Spika, taarifa iliyotolewa na wizara ya afya kuhusu rasilimali watu katika kada ya afya  kwa mwaka 1999 ilionyesha kuwa jumla ya watumishi wenye sifa 46,868 kwenye sekta ya afya walihitajika, lakini waliokuwepo ni  15,060 ambao ni sawa na asilimia 32.1% ya mahitaji yote, Upungufu wa watumishi 31,808 ambao ini sawa na asilimia 67.9%. Mchanganuo huo ulihusu mfumo mzima wa afya kuanzia ngazi ya chini hadi ya juu ya huduma za afya.[1]
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali iwaeleze watanzania toka taarifa imetolewa na Wizara na kuonyesha upungufu wa watumishi katika sekta ya afya wa asilimia 67.9% kwa mwaka 1999, sasa ni miaka 14, je ni kwa kiasi gani  imekabiliana na upungufu huo? Au taarifa zake za tafiti zinasomwa kwa wadau wa maendeleo na kuwekwa makabatini tu?

Kuendelea,Bofya Read More



Mheshimiwa Spika, Taarifa ya utafiti uliofanywa na taasisi inayojihusisha na afya ya SIKIKA, “HRH TRACKING STUDY 2012” kuhusu mahitaji ya watumishi wa afya inaonyesha kuwapo kwa upungufu mkubwa na kwamba idadi ya watumishi wanaopangiwa vituo vya kazi na kuripoti ni asilimia 70% kwa wilaya za vijijini na asilimia 93% kwa wilaya za mijini, na pia wilaya zingine hazipati watumishi kulingana na mahitaji yao.  Aidha, utafiti unaonyesha kuwa  wilaya nyingi zilipata asilimia 35% tu ya watumishi katika maombi yao. Hoja hapa ni je hiyo asilimia 30% ya  wanaopangiwa vijijini na asilimia 7% ya wanaopangiwa mijini inakwenda wapi na kwa nini? Je Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha watumishi hao wanaripoti na kufanya kazi katika mazingira rafiki?
Mheshimiwa Spika, Taarifa hiyo inaonyesha kuwa  kati ya madaktari 2252 waliopo ni asilimia 60.3% tu ndio wanajihusisha na utabibu na asilimia 39.7% wanafanya kazi tofauti kabisa na utabibu. Sambamba na hilo, inaonyesha kuwa  mgawanyo wa madaktari wahitimu (MD Graduates) ambao tafiti hiyo iliwaangaza inaonyesha kuwa ni asilimia 41.6% ya madaktari wanafanya kazi katika majiji (Mbeya, Mwanza, Arusha na Dar)  na asilimia 11.3% mikoa mingine, asilimia 36.6% haijulikani wanajihusisha na nini.  Asilimia 8.2% wanafanyakazi nje ya Tanzania.
Mheshimiwa Spika,  kwa mujibu takwimu zilizotolewa na shirika la afya la dunia (WHO)  na kuchapishwa na jarida la Joint Learning Initiative”  mwaka 2009 ,  inaonyesha kuwa kwa wastani Tanzania  kila mwaka takriban wanafunzi waliotimiza vigezo zaidi ya  1,000 wanaomba kujiunga na masomo ya udaktari, lakini nafasi zilizopo ni 200 tu.  Kulingana na taarifa kutoka kwenye utawala wa Chuo cha Afya  Bugando  ni kuwa kila mwaka wanapokea maombi  yapatayo  500 kwa ajili ya AMO lakini nafasi  zilizopo ni 50 tu kila mwaka.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inaona  kuwa kwa mgawanyo huu wa madaktari ni kweli kwamba ule Mpango wa Maendeleo wa Afya ya Msingi (MMAM) ambao ulianza rasmi mwaka 2007 na unatarajia kumalizika mwaka 2017 kila kata iwe na kituo cha afya na kila kijiji kiwe na Zahanati, ni dhahiri lengo hilo haiwezi kufikiwa.
Mheshimiwa Spika, kuna idadi kubwa ya watumishi wa afya (AMOs) ambao hufanya kazi katika Hospitali za mikoa,wilaya na mpaka vituo vya afya. Kundi hili muhimu stahili zake katika muundo wa utumishi hauonekani upo wapi, kundi hili ndio uti wa mgongo katika utoaji wa huduma za afya ukizingatia majukumu yao ya kila siku kadri wanavyoongozwa na “job description”.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inaita Serikali kueleza wazi ni nini stahili za kundi hili katika ngazi za utumishi na maslahi yao ni yapi?
Mheshimiwa Spika, aidha, kuna tatizo la wafanyakazi wanaojiendeleza mahali pa kazi wanapohitimu, kwani hawapandishwi madaraja au kulipwa stahili zao kulingana na ngazi mpya ya madaraja yao, Suala linalokatisha tama kwa wafanyakazi katika sekta ya afya. Je Serikali ina mpango gani katika kuhakikisha suala hili linapatiwa ufumbuzi wa haraka ili kutokuzidi kuleta madhara katika utoaji huduma kwenye sekta ya afya?
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na Munga na Mbilinyi (2009)[2] kuhusu sababu zinazo wafanya watumishi katika sekta ya afya kukimbilia nje ya nchi au kuhama serikalini ni utawala mbovu uliopo katika sekta ya afya ikiwa ni pamoja na upendeleo katika upandishwaji wa madaraja ya kazi, upendeleo katika kutoa fursa mbalimbali za kujiendeleza kimasomo na kimafunzo, kukosekana kwa vitendea kazi, malipo duni yasiyoendana na kazi inayofanyika. 
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani bungeni inaliona tatizo la kutokuwepo kwa usimamizi dhabiti wa sekta ya afya, kwa msingi kwamba Mganga Mkuu wa Wilaya ndiye mtawala mkuu wa sekta ya afya katika wilaya. Hili ni tatizo kubwa kwani mganga mkuu hana taaluma stahiki katika utawala wa Rasilimali watu hali inayoleta changamoto za kiutawala na usimamizi wa rasilimali watu. Ipo haja kubwa ya kuhakikisha kuwa wataalamu hawa wanapata mafunzo yatakayowawezesha kusimamia rasilimali watu. Kambi ya upinzani inahitaji maelezo ya kutosha ni jinsi gani mpango wa rasilimali watu kwa sekta ya afya kwa mwaka 2008-2013 umeweza kutatua  matatizo ya raslimali watu hapa nchini.
Mheshimiwa Spika, changamoto kubwa kwa upande wa rasilimali watu ambayo ni lazima ipewe kipaumbele ni pamoja na kuwa na Succession Plan ambayo itasaidia katika kuandaa madaktari, wauguzi na wahudumu pale ambapo wale waliopo wanakua wamestaafu, kupata matatizo, kuacha kazi ama kushindwa kuendelea na nafasi walizo nazo. Vituo vingi vya afya pamoja na hospitali, zimekumbwa na uhaba wa watumishi pale panapokua na pengo la madaktari, wauguzi ama wahudumu.
Mheshimiwa Spika, kuna suala ambalo linawasumbua sana wauguzi ambao kwa idadi kubwa ni waajiliwa wa Serikali, lakini watumishi hawa inawabidi kila mwaka katika utendaji wao walipie leseni inayowawezesha kufanyakazi zao.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inapenda kufahamu hizi leseni zinazokatwa kila mwaka fedha za leseni hizo zinapelekwa kwenye fungu lipi na ni kwanini iwe ni kada hiyo ya utumishi wa umma inayotakiwa kuwa na leseni?
2.0 HALI YA VYUO VYA MAFUNZO YA AFYA
Mheshimiwa Spika, kutokana na utafiti uliofanywa na taasisi hiyo ya SIKIKA katika vyuo vya mafunzo vya afya hamsini na moja vilivyofanyiwa utafiti mwaka 2012, inaonyesha kwama katika vyuo 30, asilimia 59 ya vyuo hivyo vilibainika kuwa na upungufu wa malazi. Na vyuo 26, asilimia 51 ya vyuo hivyo ilibainika kuwa na upungufu mkubwa wa madarasa. Aidha vyuo 24 kati ya 51, asilimia 47 vilibainika kuwa na upungufu mkubwa wa wakufunzi/walimu. Katika mtiririko huo vyuo katika 23, asilimia 45 yake vilionekana kuwa na ukosefu wa vifaa vya kufundishia.
Mheshimiwa Spika, Pamoja na mapungufu  haya yanayovikabili vyuo vya mafunzo ya watumishi wa afya, bado fedha iliyotengwa kwa maendeleo ya mafunzo ya  rasilimali watu katika sekta  ya afya kwa mwaka 2013/14 imepungua kwa asilimia 54 ukilinganisha na mwaka uliopita.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kulieleza Bunge hili ni kwa vipi mpango wa kuongeza raslimali watu kwenye sekta ya afya utaweza kufanikiwa ikiwa raslimali fedha inashindwa kuelekezwa kwenye Nyanja hiyo ya uzalishaji wataalam?
3.0 BUDGET YA MAFUNZO IDARA YA AFYA
Mheshimiwa Spika, Katika kutekeleza mpango mkakati wa rasilimali watu afya ya 2008/2013, zaidi ya shilingi bilioni 400 zilihitajika, kwa wastani kwa mwaka zinahitajika jumla ya shilingi bilioni 80. Katika mwaka wa fedha wa 2012/13 kitengo cha mafunzo afya kilitengewa jumla ya shillingi bilioni 47.6 Ambapo jumla ya shilingi Bilioni 24.3 zilitengwa kwa ajili ya matumizi ya kawaida na shilingi Bilioni 23.3 kwa ajili ya maendeleo. Mheshimiwa Spika, Kiwango hiki ni cha chini ya kiwango kilichohitajika
Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2013/14, serikali imepanga kutumia shilingi 33.9 kwa matumizi ya kawaida na maendeleo; hii ni pungufu kwa asilimia 29 ukilinganisha na mwaka wa fedha uliopita, Matumizi ya kwaida katika 2013/14 yatakuwa ni billion 23.2 (pungufu ya asilimia 5 ukilinganisha na 2012/13).
Mheshimiwa Spika, fedha za matumizi ya maendeleo kwa mwa wa fedha 2013/14 ni shilingi  billion 10.7 (pungufu ya asilimia 54 ukilinganisha na mwaka wa fedha uliopita). Kambi Rasmi ya Upinzani inauliza, ikiwa fungu la fedha zinazotengwa kwa ajili ya maendeleo ya mafunzo ya rasilimali watu katika sekta ya afya zinapungua kwa kiasi hicho, Je wafanyakazi wa kuhudumia vituo vya huduma za afya watapatikana kwa njia gani?
UAJIRI WA WATUMISHI WA AFYA UKILINGANISHA NA VIBALI VYA AJIRA
 
Mheshimiwa Spika, Pamoja na upungufu wa wafanyakazi, bado Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii imekuwa ikiajiri wafanyakazi wachache ukilinganisha na vibali vya ajira vinavyotolewa na Ofisi ya Rais– Utumishi wa umma  kama inavyoonekana katika mchoro wa umbo hapo juu.
Mheshimiwa Spika, ukiangalia mahitaji ya watumishi  walioidhinishwa kwa ajili ya kuajiriwa na idadi iliyoajiriwa  toka mwaka 2005/06 hadi 2010/2011 utaona upungufu mkubwa uliopo. Katika mwaka wa fedha 2009/10, jumla ya wafanyakazi 4,090 waliajiriwa. Idadi hii ni sawa na asilimia 65 tu ya wahitimu wa kada za afya kwa mwaka husika. Pamoja na upungufu mkubwa wa wafanyakazi, bado asilimia kubwa ya wahitimu hawakupata ajira serikalini.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inaona sasa ni muda mwafaka kwa Mheshimiwa Waziri  akaeleza  watanzania hasa wadau wa sekta ya afya ni sababu zipi zimepelekea kutolewa kwa ajira kidogo kulinganisha na idadi ya ajira ambazo zinatolewa kibali na Ofisi ya Rais  Menejimenti ya Utumishi  wa umma.
4.0 AFYA YA MAMA NA MTOTO
Mheshimiwa Spika, Sera ya afya ya mwaka 2007 inasema afya ni ukamilifu wa binadamu kimwili, kiakili na kijamii na kutokuwepo kwa maradhi. Changamoto mbalimbali zinawakumba kina mama hasa inapokuja kwenye suala zima la uzazi. Kuna uhaba mkubwa wa vifaa tiba katika hospitali na vituo vya afya katika sehemu kubwa ya Tanzania hasa vifaa vya kusaidia wajawazito wakati wa kujifungua.
Mheshimiwa Spika, aidha kuna tatizo kubwa linaloikabili nchi, ambapo wagonjwa wengi wanahitaji damu salama lakini baadhi hawapati kutokana na kutokuwepo watu wa kujitolea damu. Wagonjwa au ndugu zao hutozwa sh 2,500 kwa ajili ya kununulia mifuko ya kukusanyia damu, mirija ya dripu ya kumwingizia mgonjwa sh 2,000 na kama atakuwa anatakiwa kufanyiwa upasuaji anatoa pesa ya nyuzi sh 5,000 na kumshona ni sh 8,000,’’[3] na baadhi ya wagonjwa wanakufa baada ya kukosa msaada wa damu. Hivyo katika baadhi ya vituo vya afya na hospitali wanaamua kuokoa maisha ya wagonjwa hao kwa kuwatoa damu watu wanaokubali hasa ndugu wa wagonjwa na kuwaongezea wagonjwa bila uhakika wa vipimo vya virusi vya ukimwi (VVU) na UTI (magonjwa ya zinaa) na ini. Moja ya sababu za ukosefu wa damu kwa baadhi ya wanawake hasa kinamama wajawazito ni pamoja na ukosefu wa lishe bora ikiwamo vyakula vya virutubisho vya kuongeza damu mwilini ambapo kwa watoto ni kutokana na homa kali na malaria.
Mheshimiwa Spika, Katika kulinda afya ya mama na mtoto, kuna dawa zinazohitajika kwa wajawazito ambazo ni pamoja na za malaria, dawa za kuharakisha kupona vidonda au maumivu, SP na mseto lakini wajawazito wengi wamekuwa wakipewa dawa aina ya SP pekee huku katika baadhi ya maeneo wakinunua hata kadi za kliniki ingawa zimeandikwa kuwa haziuzwi.
Mhemshimiwa Spika, Katika kukabiliana na changamoto mbalimbali za uzazi,wajawazito wengi wamekua wakikumbana na kauli pamoja na huduma duni toka kwa wauguzi huku wauguzi wengine wakitoa kauli za kukebehi na za kukwaza ambapo  kutokana na kauli za wauguzi hao imefikia mahala wajawazito wanaona ni bora kujifungulia nyumbani au kwa wakunga wa jadi kuliko kwenda sehemu ya kutolea huduma za kisasa na kwamba watalazimika kwenda hospitali kama watakuwa na matatizo makubwa katika ujauzito wao ingawa kliniki wanahudhuria kila tarehe wanayopangiwa.
Mheshimiwa Spika, Katika karne hii ya 21, lazima Serikali iweke mikakati ya kuweza kuwaokoa wananchi wake hasa kina mama na watoto kwa kukabiliana na changamoto za sekta ya afya hasa kwa kukabiliana  na upungufu wa wauguzi na kuwatumia ipasavyo wakunga. Takwimu zilizochapishwa na ripoti ya Hali ya Wakunga Ulimwenguni (State of the World’s Midwives) zinaonyesha kuwa Tanzania inahitaji wakunga 9,941 zaidi ili kufikia lengo ifikapo mwaka 2015 la kuwa na asilimia 95% ya wajawazito wanaozalishwa na wahudumu wenye taaluma. Na kwa mujibu wa taarifa hii akina mama 5,000 na watoto wachanga 32,000 wangeweza kuokolewa ifikapo 2015. Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaitaka Serikali kueleza mipango mikakati madhubuti itakayohakikisha kuwa wakunga wanapewa nafasi katika kulinda afya ya mama na mtoto.
Mheshimiwa Spika, Kuhusu afya ya mama na mtoto, Kambi Rasmi ya Upinzani katika hotuba yake hapa bungeni 2011/2012 tulionesha wazi kutoridhika na zoezi la ununuzi wa pikipiki za miguu mitatu ambazo zilinunuliwa kwa bei ghali kwa mchakato ambao tuliulalamikia kuwa unatumia vibaya fedha za walipa kodi, masikini wa nchi hii ambao wanajitahidi kulipa kodi hizi kwa maendeleo ya taifa letu. Tulibezwa na kuitwa adui wa maendeleo. Lakini kwa wingi wa uwakilishi na demokrasia ya wengi wape hata pale maslahi ya taifa hili yanapowekwa rehani.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani bungeni inaelekeza masikitiko yake makubwa kwa Serikali kwa kununua pikipiki zaidi ya 372  kama  Mheshimiwa Waziri alivyotamka wakati wa bajeti ya afya mwaka 2012/13 lakini ukiangalia asilimia kubwa ya hizo pikipiki  zimetelekezwa katika hospitali za wilaya ama zimeshindwa kabisa kupelekwa kwenye vituo vya afya kwa kuwa miundombinu hairuhusu hizo pikipiki kutumika katika maeneo hayo.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inashindwa kuamini kuwa wakati zoezi hili la kununua pikipiki hizo wahusika wa zoezi hilo walikuwa wageni hapa nchini au kwa kuwa masuala yote yanafanyika Dar es salaam bila kujua kuna maeneo mengi ya nchi hii pamoja na miaka 51 ya uhuru bado hayawezi kufikika kwa urahisi, liwe jua au iwe mvua.  Suala hili linazidi kutia shaka kwani linapekelea uwapo wa hisia za rushwa katika zoezi hilo kutokana na msukumo ulioonyeshwa na wasimamizi wakuu wa Wizara wakati huo.
Mheshimiwa Spika, aidha, tuna inaishauri Serikali kufanya utafiti wa kutosha kabla ya kufanya maamuzi na tuache kufanya maamuzi kwa kuangalia nchi ya India au China wanafanyaje. Tukumbuke mazingira ya nchi yetu na yao nitofauti. Maamuzi kama haya mwisho wa siku yamepelekea kutumia rasilimali na kodi za walalahoi kwa vitu ambavyo havitoi tija na tatizo kuendelea kuwa sugu.
5.0 MAGONJWA YASIYOAMBUKIZA
Mheshimiwa Spika, kumekuwepo na ongezeko kubwa sana la magonjwa ya mioyo,shinikizo la damu,saratani mbalimbali n.k. Haya  magonjwa  kwa kiasi kikubwa yanatokana na kubadilika kwa hali ya maisha, aidha kwa kutokuzingatia lishe bora, kwa maana ya kutotumia vyakula asili na hatimaye kutumia vyakula vilivyosindikwa na baadhi ya kemikali.
Mheshimiwa Spika, kumekuwepo na hali ya baadhi ya watu kutopenda kufanya uchunguzi wa afya zao mara kwa mara na  na pale wanapopata maradhi hayo ambayo hutokea ghafla na kujikuta wamefikishwa hospitalini, hali inakuwa mbaya sana kwa mgonjwa.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kutoa elimu na mwongozo juu ya lishe bora na si bora lishe kuhimiza umuhimu wa watu kupima afya zao na pale inapobainika basi wapatiwe huduma za afya zinazostahili.
5.1Huduma za Macho:
Mheshimiwa Spika,kuna takriban watu milioni  285 ambao wana matatizo ya kuona Duniani. Watu milioni 39 wana upofu, watu milioni 246 wana uono hafifu, 80% ya matatizo haya yanaweza kuzuilika na 90% wapo kwenye nchi zinazoendelea.
Mheshimiwa Spika, kulingana na taarifa za shirika la afya la Dunia (WHO), Tanzania inakadiriwa kuwa na watu 992,250 sawa na 3.15% wana matatizo ya uono ambapo kati yao wasioona ni 315,000 sawa na 0.7% ya watanzania wote. Watu wenye uono hafifu wanakadiliwa kuwa 787,000, na sababu zinazoongoza ni kuwa na mtoto wa jicho (cataract), shinikizo la jicho(Glaucoma), matatizo ya retina ambayo yanatokana na sukari na umri mkubwa n,k
Mheshimiwa Spika, shughuli za utibabu huu huendeshwa na madaktari bingwa, madaktari wasaidizi au wauguzi wenye fani ya macho, na hii ni pamoja na mtaalam wa kupima upeo wa macho na miwani (optometrist).
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kueleza ina mpango gani wa kuongeza nafasi za madaktari ambao wanajiunga na vyuo vinavyotoa au kufundisha fani hii? Aidha serikali ina mpango gani wa haraka  kufanikisha uwepo wa vifaa tiba na upasusaji wa jicho katika  hospitali zetu za wilaya na mikoa? Pia  Serikali ina mkakati gani wa haraka kupitia kamati za afya ya msingi kutoa elimu sahihi ya afya katika suala la  kudhibiti upofu?
6.0 UPATIKANAJI WA DAWA, VITENDANISHI, VIFAA NA VIFAA TIBA
Mheshimiwa Spika, Suala la upatikanaji wa dawa, vifaa, vitendanishi na vifaa tiba limeendelea kuwa taizo sugu sana. Na hii inatokana na mfumo uliopo wa bohari ya madawa kufanya kazi aidha chini ya kiwango au kuendelea kufanya kazi kwa mazoea yaleyale. Sehemu nyingi upatikanaji wa dawa muhimu umekuwa ni kitendawili kisicho na jibu na hususan kwa mazingira ya vijijini na hii upelekea usumbufu mkubwa kwa wananchi wengi wasio na kipato kukosa dawa jambo ambalo ni stahili ya msingi kwa kila mwananchi. Mfano halisi ni katika hospitali ya wilaya Biharamulo, Pamoja na hoja za Serikali kuwa kumekuwa na ucheleweshaji wa maombi ya dawa, vifaa na vifaa-tiba ni ukweli usiopingika kuwa mfumo uliopo hauendani na kasi ya mahitaji ya dawa na vifaa katika maeneo mbalimbali ya nchi kutokana na ukiritimba kwenye mfumo mzima wa upatikanaji wa dawa, viaa na vifaa tiba.
Mheshimiwa Spika, Tatizo la ucheleweshwaji wa dawa pamoja na kutopatikana kwa dawa stahiki kwa wagonjwa, zimewafanya wauguzi na madaktari kubeba mzigo mzima wa lawama kutoka kwa wananchi. Mara kadhaa ucheleweshwaji wa dawa na vifaa katika vifaa vya afya umesababisha madaktari na wauguzi kuandika ununuzi wa dawa nje ya vituo vya afya. Hali hii imezua migogoro ya mara kwa mara na malalamiko mengi kwa wauguzi na madaktari kuwa wanazuia upatikanaji wa dawa, na huku serikali inaendelea kujikwepesha lawama kuwa vituo vya afya vimekua vinachelewa kuagiza dawa na hivyo mzigo wa lawama umekua mkubwa kwa wauguzi na hivyo kuleta uhasama kwao na wananchi na mpaka sasa ni ukweli kuwa wananchi hawana imani na vituo vya afya pale wanapoambiwa kuwa dawa na vifaa havipatikani.
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa taarifa ya utafiti iliyotolewa mwezi wa march 2012  na taasisi isiyo ya kiserikali inayojihusisha na afya ya SIKIKA kuhusu,  “Availability of Essential Medicines,Medical Supplies and Bed Capacity in Hospitals in Tanzania Mainland”  ambao ulihusu hospitali 54 za Serikali uligundua kwamba  kati hospitali hizo  43 zilikuwa ni hospitali za wilaya  na kati ya hospitali hizo za wilaya  40 zilichaguliwa “randomly” na tatu zilizobaki zilichaguliwa kwa vigezo maalum  kwenye maeneo ambayo taasisi hiyo inafanyia kazi. Aidha, 11 zilizobaki zilikuwa ni hospitali za rufaa za mikoa.
Mheshimiwa Spika, matokeo ya utafiti huo ni kwamba 94% ya hospitali hizo zilionyesha kukosekana kwa madawa na vifaa tiba  “out of stock of one or more essential medical supplies”, 96%  ya hospitali zilionyesha kukosekana kwa madawa muhimu. Aidha,taarifa hiyo inaonyesha kuwa vifaa tiba ambavyo vimekuwa ni tatizo kwa takriban hospitali zote ni: gloves imeonyesha 83% , sutures (48%), gauze (39%) for medical supplies, and quinine (43%) and metronidazole (31%) for medicines. Asilimia , 52% na  59% ya hospitali zilionyesha kuwa zilikuwa zinaishiwa madawa na vifaa tiba  muhimu  kwa kipindi kinachozidi majuma manne.
Mheshimiwa Spika, kwa kuangalia takwimu za utafiti huo ni dhahiri sekta hiii ya madawa na vifaa tiba kwa hospitali zetu bado ni tatizo kubwa, na Kambi ya Upinzani inashindwa kuelewa kwa mwendo huo ni kwa jinsi gani malengo ya millennia yatafikiwa? Tunamtaka Mhe Waziri awape ufafanuzi watanzania tatizo hilo kwa sasa limetatuliwa kwa kiwango gani.
Mheshimiwa Spika, Kwa upande wa  dawa na vifaa tiba hali ni mbaya zaidi kutokana na ukweli kwamba kutokana na makadirio ya fedha shilingi bilioni 198 katika mwaka wa fedha 2012/13 zilizotakiwa kwenda Bohari kuu ya madawa kwa ajili ya kufanya manunuzi ya dawa na vifaa  hadi mwezi Desemba 2012 zilikuwa zimetolewa shilingi bilioni 3 sawa na takriban asilimia 3; na hadi mwezi  Machi 2013 zilikuwa zimetolewa shilingi bilioni 28.3 ambayo ni takribani asilimia 27 ya bajeti iliyokuwa imetengwa kwa taasisi hiyo.
7.0 BOHARI YA DAWA YA TAIFA (MSD)
Mheshimiwa Spika, Tunataka taifa lijue kuwa Serikali ya CCM inacheza na uhai na afya zao. Pamoja na changamoto mbalimbali ambazo MSD inakumbana nazo, pamoja na makelele ya taifa kuwa hakuna dawa za kutosha kwenye vituo vya afya huku viongozi wa Serikali wakiendelea kufanya manunuzi kwa magari yenye thamani kubwa na safari za nje zisizo kuwa na uratibu au tija. Huku wakielewa kuwa Bohari ya Dawa inaidai Serikali kiasi cha sh. bilioni 52 ambazo zimelimbikizwa kutokana na madeni ya muda mrefu ya huduma za dawa, vifaa, na vifaa tiba ambavyo taasisi hiyo ilitoa kwa vituo vya afya vya Serikali pamoja na hospitali zake.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaishauri Serikali kuangalia upya vipaumbele vyake kwani afya ya watanzania inatakiwa kuwa ni kipaumbele cha msingi badala ya utaratibu mpya wa ulaji kwa ofisi ya Rais wa uanzishwaji wa kinachoitwa Presidential Delivery Bureau, na kutenga shilingi bilioni 28 kwa ajili ya  vikao tu.
Mheshimiwa Spika, Leo tunaongelea ucheleweshaji wa utoaji wa fedha kwa MSD unaosababisha pia kuharibu na  kucheleweshwa kwa mfumo mzima wa manunuzi na usambazaji wa madawa na vifaa tiba kwa nchi. Aidha, kwa mfuatano huo ni kwamba uboreshwaji mzima wa sekta ya afya unazidi kuwa mgumu sana na hivyo kushindwa kutimiza malengo ambayo tunajiwekea kama nchi. Afya za wananchi wa taifa hili, Serikali ya CCM imeziweka rehani. Lazima kama taifa tuseme, lazima tukatae ujanja ujanja wa Serikali hii.
Mheshimiwa Spika, Bohari ya Dawa ina changamoto mbalimbali inazokumbana nazo, zikiwemo za vyombo vya dola kuwafumbia macho baadhi ya wafanyabiashara wanaouza dawa za serikali kiholela pamoja na wanaokamatwa kwa kutorosha dawa hizo nje ya nchi. Taasisi zilizomwagiwa lawama hizo ni baadhi ya maofisa kutoka vyombo vya dola, serikalini na wafanyabiashara. Hayo yalisemwa na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bohari ya Dawa (MSD), Cosmas Mwaifwani  wakati wa Kongamano la Nane la Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) la kujadili tafiti zilizofanywa na wanahabari kuhusu matumizi ya fedha zinazochangwa na wananchi kwa ajili ya masuala ya afya katika halmashauri 26 nchini.
Mheshimiwa Spika, Pamoja na hayo bado kuna tatizo kubwa la kutoainisha pesa inayotengwa kwa ajili ya madawa, vifaa tiba vitendanishi inayopelekwa Tamisemi. Kumekuwapo utendaji ambao ki-msingi unaongiliana lakini hakuna usimamizi wa jumla wa wizara hizi mbili. Kambi Rasmi ya Upinzani inatoa wito kuwepo na Afisa wa Wizara ya afya atakaye simamia mipango ya Afya upande wa TAMISEMI.
8.0 MAMLAKA YA CHAKULA NA DAWA TANZANIA (TFDA)
Mheshimiwa Spika, Mamlaka ya chakula na dawa, iliyopo chini ya wizara hii, ilianzishwa kwa ajili ya kuimarisha udhibiti wa ubora na usalama wa vyakula, vipodozi na vifaa tiba nchini ili kulinda afya za watumiaji. Kati ya majukumu yake ni pamoja na kudhibiti utengenezaji, usambazaji na uuzaji wa dawa, vipodozi na vifaa tiba; ukaguzi wa viwanda vya utengenezaji; kufuatilia madhara yatokanayo na matumizi ya dawa zinazodhibitiwa; kufanya uchunguzi na uhakiki wa ubora na usalama wa bidhaa na kadhalika.
Mheshimiwa Spika, Katika kutekeleza wajibu wake wa uchunguzi wa sampuli za bidhaa kimaabara, jumla ya asilimia 83.5 zilifaulu uchunguzi. Pamoja na TFDA kuzuia bidhaa zilizoshindwa vigezo kuingia nchini au kusitishwa matumizi ya bidhaa na kuondolewa kwa bidhaa hizo sokoni, haijatoa taarifa rasmi ya uchunguzi wa madhara ya bidhaa ambazo tayari zilikua sokoni na kusababisha madhara kwa watumiaji, na kama watumiaji walioathirika na bidhaa zisizokidhi vigezo. Hivyo Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, inaitaka wizara kulieleza Bunge lako jumla ya idadi ya waathirika wa bidhaa zisizokidhi vigezo ambao wamelipwa fidia kufikia Machi mwaka huu.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaendelea kusisitiza kuwa ili kuwe na na mfumo udhibiti bora wa dawa, chakula, vipodozi na vifaa tiba lazima kuwe na sheria madhubuti zenye kuendana na uhalisia wa hali ya sasa yenye changamoto nyingi. Kambi rasmi ya Upinzani Bungeni inaishauri Serikali kuharakisha marekebisho ya Sheria ya Chakula, Dawa na Vipodozi ya mwaka 2003 ambayo imepitwa na wakati hivyo kuleta changamoto katika utendaji wa Mamlaka ya Chakula na Dawa.
Mheshimiwa Spika,  Katika kaguzi za huduma za afya nchini, ripoti zinaonesha kuwa kumekuwepo na udanganyifu wa sifa na ujuzi kwa watumishi wa kada ya wauguzi na wahudumu pamoja na watumishi wengine kupata mshahara bila ya kufanya kazi. Pamoja na mikakati ya wizara katika kukabiliana na changamoto hii, kwa kuwahimiza waajiri kuthibitisha sifa za wataalamu wao kwenye mabaraza ya kitaaluma bado mfumo uliopo nchini, haujaweza kudhibiti vitendo vya kugushi sifa za kitaaluma hivyo kufanya zoezi zima la kudhibiti ongezeko la vitendo hivyo kuwa gumu. Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, inataka majibu kutoka kwa waziri kutoa kwa kutoa kiujumla idadi ya watumishi ambao wamegushi sifa na ujuzi wao na majibu ya hatua zilizochukuliwa na Serikali katika kuhakikisha kuwa mapungufu haya hayajitokezi katika sekta ya afya ukizingatia kuwa Sekta ya Afya nchini, ni sekta muhimu hivyo kuwa na watu waliogushi ujuzi na sifa stahiki katika utoaji wa huduma za afya ni kuhatarisha maisha na kuziweka rehani afya za wananchi.
9.0 TATIZO LA DAWA BANDIA ZA KUPUNGUZA MAKALI YA UKIMWI (ARVs) NCHINI
Mheshimiwa Spika, taarifa kwamba watu 5,358 wanaoishi na Virusi vya UKIMWI (VVU) waliokuwa kwenye matibabu wameacha kutumia dawa za kupunguza makali ya ugonjwa Huo (ARVs), mkoani Dodoma. Taarifa kupitia vyombo vya habari na taasisi mbalimbali kuhusu  watu wanaoishi na Virusi vya UKIMWI (WAVIU) kuacha kutumia dawa, zimekuja kipindi ambacho Wananchi na wadau wa UKIMWI wakitafakari hatma ya uchunguzi wa sakata la kutengenezwa  Dawa bandia za ARVs.
Mheshimiwa Spika, Dawa hizo aina ya TT--VIR toleo namba (batch number oc.01.85) zilisambazwa katika mikoa ya Mara, Tanga na Dar es Salaam tangu Mei, 2011. Kuwepo kwa ARVs bandia na taarifa juu ya WAVIU kuacha kutumia dawa kunadhihirisha Udhaifu uliopo ndani ya mifumo na mamlaka za serikali zilizopewa kusimamia ubora, Uwepo na upatikanaji wa dawa. Inaaminika, kuwepo kwa uhusiano wa karibu kati ya uwepo wa dawa hizo bandia nchini Na WAVIU hao kuingiwa hofu na kuacha kutumia dawa.
Tunaamini hayo kwa kuzingatia ukweli kwamba suala la mgonjwa kutumia dawa kwa kiasi kikubwa Linategemea imani na utayari wa mhusika.
Mheshimiwa Spika, uwepo wa dawa bandia ama zisizo na ubora unapunguza imani na hivyo kuweza kusababisha mgonjwa kuacha kuzitumia na kupelekea kuathirika zaidi.
Sakata la kuwepo kwa ARVs Bandia lililochukua takribani miezi nane sasa, limekuwa na sura tofauti Hususan juu ya nani anahusika moja kwa moja baada ya kiwanda kinachodaiwa kutengeneza dawa Hizo Tanzania Pharmaceticals Industry (TPI) kukanusha kuhusika na utengenezaji huku Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) na Bohari Kuu ya Dawa (MSD) wakisisitiza kuwa dawa hizo zimetoka kiwandani hapo.
Mheshimiwa Spika, Pamoja na kuwa uchunguzi unaendelea kuhusu dawa hizi lakini waathirika wa ugonjwa wa UKIMWI waliopata madhara ya dawa hizi wengine wameshapoteza maisha, wengine wameendelea kudhoofika na pia imefanya idadi kubwa ya waathirika kupuuzia dawa nyengine za ARVs kwa kuhofia kuwa zitaleta madhara zaidi. Pamoja na yote hayo bado Serikali kwa kupitia timu ya wataalamu iliyoundwa kwa lengo la kufuatilia tiba na matunzo kwa wagonjwa wa UKIMWI, imetoa matokeo ya awali ya ufuatiliaji wa madhara ya dawa hiyo ya bandia ya TT-VIR 30 toleo Na. OC.01.85 kuwa hayakubaini wagonjwa waliodhurika kwa kutumia kwa kutumia dawa hiyo. Kambi Rasmi inapingana na matokeo haya ya awali kwa kuwa inao ushahidi kuwa wapo watanzania, wenzetu walioathirika kwa matumizi ya dawa hizo za bandia.
Mheshimiwa Spika, Kwa mujibu wa taarifa kutoka ofisi ya DPP, jalada la kesi ya ARVs bandia limepokelewa na linashughulikiwa ili kupata muelekeo wa nani ahusishwe na kwa kosa gani kabla ya kuachia mamlaka husika jukumu la uchunguzi wa kina. Kwa maelezo ya ofisi hiyo, Suala la ARVs bandia limechukua muda mrefu (zaidi ya miezi miwili), tofauti na muda wa kawaida wa siku 14 unaotumiwa na ofisi ya DPP kushughulikia kesi mbalimbali zinazofikishwa hapo, kutokana na uzito/unyeti wa suala hilo.
Mheshimiwa Spika, Wakati taratibu hizo za kitaalamu na kisheria zikiendelea, tunaishauri Serikali kutoa taarifa rasmi kwa wananchi juu ya dawa bandia (makopo 4,000) ambazo hazijakusanywa. Je, ziko vituoni au zilishatumiwa na wananachi? Kama zilishatumiwa, je serikali ina taarifa zozote Juu ya waliozitumia dawa hizo? Je, kuna madhara yoyote waliyopata kutokana na kuzitumia?
Kwa kutoa taarifa sahihi, serikali itasaidia kuwatoa mashaka wanaotumia ARVs na kuwajengea imani waendelee kuzitumia bila kuathiri afya zao.
Mheshimiwa Spika, Mwaka 2010, mkoani Arusha iliripotiwa kuwa kuna dawa ambazo ziliisha muda wake wa matumizi za kupunguza makali ya UKIMWI ambazo zilileta madhara kwa watumiaji ambazo zilikua zikitolewa na kituo cha Matibabu cha Arusha Lutheran Medical Centre. Ndugu Joseph Lukumay, ambaye ni mkazi wa kata ya Kioga, Meru pamoja na wengine walilalamikia kupewa ARVs aina ya Efavirenz zilizotengenezwa na Aurobindo Pharma Limited ya India. Pamoja na muda wa kutengenezwa dawa ilikua ni Januari 2008 na zilitakiwa zitumike kabla ya Disemba 2009, ALMAC ilianza kuzitoa hizo dawa kuanzia Januari 2010 na kuendelea. Pamoja na wagonjwa hawa kulalamika kuwa dawa hizo zimekwisha muda wake, walipata majibu toka ALMAC kuwa dawa hizo hazitaleta madhara ikiwa zitatumika ndani ya miezi sita ya kwanza baada ya siku yake ya matumizi kuisha. Baada ya kutumia ndani ya miezi mitatu, dawa hizo zilianza kumletea madhara Ndugu Lukumay kwa kumbabua ngozi, kumtoa vidonda  na malengelenge ambapo pamoja na kuripoti ALMAC, alipewa vitisho na kusitishiwa matibabu yake.
Mheshimiwa Spika, Ingawa pamoja na maelekezo ya Serikali ya kuagiza dawa zote za matibabu lazima ziagizwe na kusambazwa na MSD, baadhi ya vituo vyenye mrengo wa kiimani vimekua vikitumia mianya iliyopo katika kuingiza dawa na vifaa kinyume na taratibu zilizowekwa kwa kuwa huwa wanapata misaada kutoka mashirika ya nje ya nchi.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inataka kujua mkakati ambao umewekwa na Wizara kwa mwaka 2013/2014 kwa ajili ya kuhakikisha kuwa vituo vya afya vinavyopata misaada toka kwa mashirika ya nje ya nchi yanatimiza taratibu za kuingiza nchini misaada ya kitiba hapa nchini. Aidha, tunataka Serikali itoe kauli juu ya tuhuma zilizotolewa dhidi ya ALMAC ili kuweza kuwasaidia waathirika wa UKIMWI katika kupata haki zao hasa pale inapotokea madhara yanayosababishwa na uzembe wa vituo vya afya katika matibabu yao.
10.0 MWENENDO WA TIBA ASILIA NA TIBA MBADALA NCHINI
Mheshimiwa Spika, TANZANIA ina idadi kubwa ya miti ya aina nyingi inayoweza kutumika kama tiba ya maradhi mbalimbali.Inakadiriwa kuna aina 15,000 za miti inayotumika kama dawa nchini, lakini Watanzania hawafaidiki na mauzo ya dawa zenyewe, yanayokadiriwa kuingiza Dola za Marekani bilioni1.6 kwa mwaka.
Mheshimiwa Spika, umuhimu wa dawa za zinazotokana na miti, unajionyesha hasa kwa kuwa asilimia 60 ya Watanzania hutegemea tiba asili kwa matibabu yao. Tanzania inayo nafasi kubwa ya kujitajirisha kwa kuuza dawa asilia. Kati ya vigezo vya soko la dawa hizo kuwa ni dawa kuwa na virutubisho vinavyotakiwa, ziwe zimetafitiwa kisayansi ili kuonekana kama hazina sumu na kuweka mbinu za biashara kwa dawa hizo.Kwa Tanzania, dawa za miti hutathminiwa na kusajiliwa na Mamlaka ya Chakula na dawa (TFDA) kabla ya kuanza kuuzwa. Lengo la kuhakiki na kusajili ni kuhakikisha usalama, ubora kwa ajili ya matumizi ndani ya nchi.
Mheshimiwa Spika, kutokana na umuhimu wa tiba asilia, Serikali ilitunga sheria namba 23 ya mwaka 2002 ili kuratibu utendaji mzima wa sekta hii. Wizara ya Afya itoe takwimu kuna watabibu wangapi waliosajiliwa na wangapi bado kusajiliwa kulingana na matakwa ya sheria hii.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali iwaeleze wadau katika sekta hii imeweka mkakati gani wa kuielimisha jamii juu ya tofauti za waganga wa kienyeji, waganga wa tiba asili, waganga wa jadi na watibabu wa Tiba mbadala. Utaratibu gani umewekwa kisheria kuwasajili waganga wa tiba asili, kwani usajili wa wahusika unatakiwa uanzie ngazi ya mtaa hadi taifa. Hivi ni chombo gani kina hakikia uhalisia wa wanaosajiliwa, aidha, kuna tatizo pale waganga wa tiba asilia wanapoambiwa wachangie kiasi cha Shilingi 80,000 hadi 200,000/- za kikao. Je, ni kweli utaratibu huu unasaidia kuimarisha huduma za afya zitolewazo na tiba asili.
Mheshimiwa Spika, kutokana na kukua kwa soko la tiba asili duniani na nafasi ambayo Tanzania inayo katika kunufaika na soko hilo, ambalo nchini Cameroon peke yake kwa kutumia soko la tiba asili iliweza kuingiza Dola milioni 40 mwaka 1993 kwa kuuza mti ujulikanao kwa jina la ‘Prunus Africana’ na mbegu za ‘Voacanga Africana’ unaoaminika kutibu magonjwa ya uzee, pekee. Hivyo kambi rasmi ya upinzani bungeni, inaitaka Serikali kwa kupitia kwa waziri mwenye dhamana ya wizara ya  afya na ustawi wa jamii, alieleze bunge lako tukufu, ni mikakati ipi ambayo imewekwa kwa mwaka huu wa fedha wa 2013/2014 katika kuhakikisha kuwa taifa linanufaika kwa soko la miti ya tiba asilia.
Mheshimiwa Spika, Kambi rasmi ya Upinzani Bungeni, inajua kuwa licha ya kuwepo kwa soko kubwa la dawa hizo na kuwa na sheria kama vile Sheria ya NIMR namba 23 ya 1979, sheria ya dawa za jadi na nyinginezo na sheria iliyoanzisha TFDA ya mwaka 2003, bado Tanzania haifaidiki na soko hilo. Kati ya mambo ambayo yanaleta changamoto katika uendelezaji wa tiba asili nchini ni udhaifu wa tafiti nchini, ampapo taasisi kama NIMR, ITM, TAFORI na TAWIRI hazipati misaada ya kutosha katika tafiti zake.
Mheshimiwa Spika, kuna tatizo kubwa kwani Serikali imeshindwa kusimamia sheria hii, kwani dawa zinasambazwa kiholela kila mtu anajiita mganga wa tiba asilia. Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali iwathibitishie watumiaji wa huduma hii usalama wa madawa hayo?
Mheshimiwa Spika, Kutokana na kukua kwa soko la tiba asili duniani na nafasi ambayo Tanzania inayo katika kunufaika na soko hilo, ambalo nchini Cameroon peke yake kwa kutumia soko la tiba asili iliweza kuingiza Dola milioni 40 mwaka 1993 kwa kuuza mti ujulikanao kwa jina la ‘Prunus Africana’ na mbegu za ‘Voacanga Africana’ unaoaminika kutibu magonjwa ya uzee, pekee. Hivyo kambi rasmi ya upinzani bungeni, inaitaka Serikali kwa kupitia kwa waziri mwenye dhamana ya wizara ya  afya na ustawi wa jamii, alieleze bunge lako tukufu, ni mikakati ipi ambayo imewekwa kwa mwaka huu wa fedha wa 2013/2014 katika kuhakikisha kuwa taifa linanufaika kwa soko la miti ya tiba asilia.
Mheshimiwa Spika, kuna watu wanaotoa uchawi maarufu kama rambaramba ambao kutokana na taarifa zisizo rasmi kuwa mratibu wake anajulikana na vyombo vya dola. Watu hawa wamesababisha hujuma na hasara kubwa sana kwa jamii kwa nyumba kuchomwa moto, watu kupoteza maisha. Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kutoa kauli kuhusiana na mtandao huo ambao mratibu wake ni maarufu kwa vyombo vya dola.
11.0 KIKOMBE CHA BABU WA LOLIONDO
Mheshimiwa Spika, Kati ya jambo ambalo lilileta gumzo katika sekta ya afya ni pamoja na tiba ya asili maarufu kama 'Kikombe cha Babu wa Loliondo' iliyokua ikitolewa na Mchungaji mstaafu wa Kanisa la Kiinjili la Kiluteri Tanzania (KKKT), Ambilikile Mwasapila.
Mheshimiwa Spika, Viongozi waandamizi wa Serikali, walifurika Loliondo kwa babu na hivyo kuzidisha imani kwa wananchi kuwa tiba ile ilikua ni sahihi na ya kuaminika. Wananchi wengi, wakiwemo wabunge walikimbilia Loliondo kwa kuwa Serikali iliingilia "uvumbuzi wa kiboko ya magonjwa' na wagonjwa kupuuza matibabu ya hospitali. Safari ya kwenda Loliondo ilizua matumaini mengi kwa wananchi, huku Serikali kabla ya kufanya utafiti wa kina wa  ubora wa dawa hii katika kutibu magonjwa sugu. Pamoja na majibu haya ya Serikali ya 'kikombe cha babu' kuashiria kuwa haina madhara, haikutoa majibu ya kitaalamu ya uwezo wa dawa ile kwa wakati ule katika tiba ya magonjwa sugu ambapo hata wakati ule kuna mawaziri waliofuata ‘tiba’ hiyo ya Babu ambao nao walichangia mno kuwaaminisha mamilioni ya Watanzania kuwa tiba hiyo ya Babu ni ya kweli. Leo hii, kuna watu wengi ambao wamefariki kutokana na 'kikombe cha babu'. Kuna waliofariki wakiwa njiani kuelekea kwa babu, kuna waliofariki wakiwa kwa babu, na kuna waliofariki hata baada ya kunywa 'kikombe cha babu'. Na kwa mujibu wa aliyekuwa waziri wa afya na ustawi wa jamii, Mh. Dr. Haji Mponda, alisema kuwa jumla ya watu 116 walifariki kutokana na sababu mbalimbali wakiwa kijijini Samunge au wakitoka kituo cha Arusha kupitia Mto wa Mbu na Bunda kupitia Serengeti wakielekea kwa Babu kupata kikombe. Mpaka leo Serikali haijasema chochote kuhusu uchunguzi wa dawa ya babu. Mpaka leo Serikali haijatoa kauli yoyote na wala kuchukua hatua yoyote dhidi ya Mzee Masapila ambaye Februari hii alitoa kauli nyengine juu ya ugunduzi wa dawa nyengine.
Mheshimiwa Spika, Timu ya uchunguzi iliyoundwa mpaka mwezi machi 2011 ilikuwa imeandaa kukamilisha  taratibu, ili kufuatilia  maendeleo ya kiafya ya wagonjwa 200, ambao wamekubali kwa ridhaa yao wenyewe, kushiriki katika utafiti huu, ili kuona maendeleo yao kiafya, baada ya kunywa dawa ya Mchungaji mstaafu Ambilikile Masapila, kwa maradhi walionayo, kwa kufuata vigezo vyote vya Kitaifa na Kimataifa.
Mheshimiwa Spika, naomba kutoa nukuu ya Kaimu Mkurugenzi wa Mamlaka ya Chakula na Dawa Tanzania (TFDA), Charys Ugullum, na timu ya wataalamu iliyoanza utafiti wake wa awali Machi 7, 2011, timu hiyo ilijumuisha wataalamu kutoka Wizara ya Afya, TFDA, Taasisi ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR), Mkemia Mkuu wa Serikali na Taasisi ya Utafiti wa Dawa za Asili ya Chuo Kikuu cha Afya ya Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS), kwamba;     "Serikali imesema imeridhishwa na dawa inayotolewa na Mchungaji Ambilikile Mwasapila wa Kijiji cha Samunge, Loliondo ikisema haina madhara yoyote kwa matumizi ya binadamu,”
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inatoa ushauri kwa serikali kwa kuanzisha taasisi ya kitaifa itakayoweka takwimu za dawa za asili na kuibua mipango itakayohamasisha wananchi katika tiba asili pamoja na kujengewa uwezo na kuwezeshwa katika sekta hii; pia kuongezwa kwa viwanda vitakavyozifanya dawa hizo kuwa za kibiashara, na kuimarisha ushirikiano kati ya sekta binafsi na zile za umma; kufanya uchambuzi yakinifu na tafiti za kuinua sekta ya miti ya tiba asili kwa kuainisha mikoa na sehemu ambazo zina miti ya tibaasili itakayoenda sambamba na upandaji wa miti ya dawa kwa ajili ya biashara kama vile milonge, Artemisia annua; kuwepo kwa mipango mikakati ya kuinua  teknolojia na uwekaji ubora wa dawa hizo na kuitunza miti hiyo ya dawa. Tukifanya hivyo, dawa za asili zitaleta ajira na kukuza uchumi wa nchi yetu.
12.0 USIMAMIZI WA FEDHA KWA MIRADI MISONGE
Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kupitia wizara hii ilianzisha mfumo wa kielektroniki wa ukusanyaji wa taarifa za mapato na matumizi ya fedha kwa miradi misonge ambayo ni Mradi wa Kifua Kikuu, UKIMWI na Malaria kwa mwaka 2011/2012. Mfumo huu unawezesha kutoa ripoti kwa wakati kulingana na mahitaji, hivyo utatumika pia kwenye miradi mingine. Aidha, Hospitali za Rufaa Mbeya na KCMC zimeanza kutumia mifumo ya aina hiyo katika shughuli mbalimbali za ukusanyaji wa taarifa za hospitali; zikiwemo taarifa za fedha, huduma za wagonjwa pamoja na za kiutawala. Kambi rasmi ya Upinzani inataka takwimu rasmi ya jumla na idadi ya hospitali zenye miradi misonge iliyopo sasa na mafanikio na changamoto za mfumo huo na mikakati ya Wizara kwa mwaka huu wa fedha wa 2013/2014 katika kuhakikisha kuwa mfumo huu wa kielektroniki unasambaa nchi nzima.
13.0 HOSPITALI ZA MIKOA 
Mheshimiwa Spika, ni vizuri fedha zinazotengwa kwa ajili ya afya zikatumika ipasavyo kwani afya ndo msingi bora wa maisha ya watanzania, kwa mwaka wa fedha 2013/14  fedha zilizotengwa kwa ajili ya hospitali za mikoa ni bilioni 65 ikilinganisha na kiasi cha bilioni 68 zilizotengwa kwa ajili ya matumizi ya kawaida na kwa ajili ya fedha za maendeleo.Kambi ya upinzani inahitaji majibu ya kutosha kutoka serikalini ni kwa nini fedha zinatengwa kidogo kwenda kwenye mikoa ili hali ndo sehemu ambazo watanzania wengi wanaishi na kufanya shughuli zao za maendeleo.
Mheshimiwa Spika,Kwa mwaka wa fedha 2013/14 fedha zilizotengwa kwa ajili ya ujenzi wa hospitali za mikoa ni takribani kiasi cha bilioni tatu fedha hizi zimetengwa kwa ajili ya mikoa ya singida pwani  na manyara. Kambi ya upinzani inashauri ujenzi wa hospitali za mikoa zitengewe fedha nyingi na kwa wakati il;I kuweza kufanikisha ujenzi kwa haraka na wananchi waweze kupata hudumu kwa wakati muafaka .Kukamilika kwa wakati kwa ujenzi wa hospitali za mikoa zitasasidia kupunguza mzigo mkubwa wa wagonjwa unaozikikumba hospitali za  wilaya hivyo kufanya watu wengi kukimbilia hospitali kuu za kitaifa kama muhimbili ili hali matatizo yao yangeliweza kutatuliwa katika ngazi ya mkoa.
14.0 AFYA NA USAFI WA MAZINGIRA
Mheshimiwa Spika, ni wazi kuwa pamoja na kuendeshwa kwa mashindano ya afya na usafi wa mazingira yanayohusisha Halmashauri zote nchini, tatizo la uchafu wa mazingira ambao ni hatarishi kwa afya za wananchi. Pamoja na kuwa mashindano hayo kuwa na zawadi mbalimbali katika kila kundi ili kuhamasisha wadau mbalimbali katika shughuli za usafi wa mazingira kwa washindi wa kila kundi lakini Serikali kwa kupitia wizara hii inashindwa kuelewa kuwa, changamoto si kutoa zawadi kwa washindi wa mashindano ya usafi wa mazingira bali ni nini kinafanyika kwa halmashauri zinazoshindwa katika utunzaji na usafi wa mazingira. Ni jambo la ajabu kuwa mashindano yanafanyika kuwazawadia wasafi lakini hakuna adhabu kwa halmashauri chafu jambo linalofanya usafi wa mazingira kuonekana si kipaumbele kwa halmashauri.
15.0 MWENENDO WA BAJETI YA AFYA NA USTAWI WA JAMII
Mheshimiwa Spika, Kama ilivyo kawaida hali ya bajeti imekuwa katika sura ileile ya kutengewa fedha kidogo ambazo hazikidhi mahitaji.Hakika bila ya kuwa na afya ya kutosha huwezi kuwa na mipango yoyote endelevu. Bado bajeti yetu haijakidhi hata kidogo azimio la Abuja la kutenga kiasi cha 15% ya fedha zetu za ndani kwa ajili ya bajeti ya afya. Kwa miaka mitatu mfululizo bajeti ya afya imekuwa imetengewa kama ifuatavyo; kwa mwaka wa fedha wa 2010/2011 (12.1%), 2011/2012 (10.4%), na 2012/2013  (10.4%)
Mhesimiwa Spika, Bajeti ya wizara ya afya na ustawi wa jamii imeongezeka kutoka kiasi cha shilingi 576 bilioni hadi kiasi cha shilingi bilioni 748 hili likiwa ni ongezeko la asilimia 29.9  lakini ukiangalia kwa makini utagundua kuwa  kuwa bajeti ya afya imekuwa tegemezi kwa kiasi kikubwa. Kwa mwaka wa fedha 2013/14 Serikali imetenga bilioni 36 tu kwa fedha za maendeleo ilhali tukitegemea kiasi cha bilioni 435 kutoka kwa wahisani. Kambi Rasmi ya upinzani inahitaji majibu ni kwa nini kila mara utegemezi unakuwa mkubwa hali inayoweka maendeleo ya afya na ustawi wa nchi yetu rehani endapo wahisani watajitoa katika kufadhili miradi ya maendeleo.
Mheshimiwa Spika, Japokuwa, tumekua tukitenga fedha kwa ajili ya Wizara ya Afya na ustawi wa jamii bado fedha tunazotenga hazitolewi kwa wakati na hivyo kufanya wizara kushindwa kutekeleza majukumu yake ipasavyo. Mwaka wa fedha 2012/13 bunge lako liliidhinisha kiasi cha shilingi bilioni 581 kwa ajili ya wizara lakini cha kushangaza hadi mwezi Machi mwaka huu kiasi cha bilioni 325 zilipokelewa na wizara ikiwa ni asilimia 66.6 ya fedha zote zilizotengwa.
Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani Bungeni inahitaji maelezo ni kwa nini Serikali inashindwa kutoa fedha zilizoidhinishwa kwa mwaka 2012/13. Serikali ilitenga kiasi cha bilioni 19 kama mchango wake katika fedha za maendeleo lakini hadi Machi 2013, Serikali ilitoa tu kiasi cha  bilioni 12 tu; hiki ni kitendo cha kustaajabisha. Hata hivyo Serikali yetu, sikivu, imeshindwa kutoa fedha za maendeleo kwa wakati na sasa tunahoji tunapeleka wapi mustakabali wa afya na ustawi wa taifa letu.
Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo kwa niaba ya Kambi Rasmi ya Upinzani, naomba kuwasilisha.
……………………………………..
Dr. Antony G. Mbassa (Mb)
Msemaji Mkuu wa Kambi Rasmi ya Upinzani-Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii
08.05.2013 
 
Chanzo:CHADEMA social media.

No comments:

Post a Comment

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...