Thursday, March 28, 2013

MANJI NA MWALUSAKO WAJISALIMISHA MAHAKAMA KUU

Mwenyekiti wa Yanga Yusuph Manji akiongea na waandishi wa habari
 MWENYEKITI wa Yanga, Yusuph Manji na Katibu wake, Laurence Mwalusako, wamejisalimisha Mahakama Kuu Kitengo cha Kazi ili wajieleze kwa nini wasifungwe jela kwa kukaidi amri ya mahakama.

Viongozi hao walijisalimisha jana, mbele ya Msajili wa mahakama hiyo, Mohammed Gwaye, baada ya kutakiwa kufanya hivyo kwa sababu walishindwa kuwasilisha mahakamani hapo dhamana ya Sh 106,300,000.

Gwaye aliwaamuru kuwasilisha dhamana hiyo wakati wakisubiri hatima ya marejeo ya uamuzi uliotolewa na Kamisheni ya Usuluhishi wa Migogoro, iliyowataka Yanga kuwalipa wachezaji waliowafukuza jumla ya Sh 106,300,000 kwa kuvunja mikataba yao kinyume cha sheria.

Wachezaji hao ni Steven Malashi na Wisdom Ndlovu kutoka Malawi, waliochukuliwa na Yanga kwa mkataba wa miaka miwili wakati wakijiandaa kwa kipindi cha Ligi Kuu.

Malashi na Ndlovu walikimbilia Kamisheni ya Usuluhishi, mgogoro wao ulisikilizwa huku Yanga wakigoma, ambapo Mahakama iliamuru Ndlovu alipwe Sh milioni 57, zikiwa ni mishahara ya miaka miwili, Sh 1,800,000 gharama za usafiri kutoka Malawi, Sh milioni 20 fidia, wakati Malashi aliamuliwa kulipwa Sh milioni 18 za mshahara wa miaka miwili, Sh milioni 10 fidia na Sh 500,000 fedha zake za usajili zilizobaki kwa mwaka 2009 na 2010.

Msajili wa Mahakama Kuu Kitengo cha Kazi, Mohammed Gwaye, alitoa uamuzi wa maombi hayo Februari 4 mwaka huu, akiamuru Yanga kuwasilisha fedha hizo mahakamani wakati wakisubiri hatima ya marejeo, lakini hawakufanya hivyo hadi ilipotolewa amri ya kuitwa mahakamani kueleza kwa nini wasifungwe jela kwa kushindwa kutekeleza amri ya mahakama.

Manji na Mwalusako walifika mbele ya Msajili Gwaye kwa ajili ya kujieleza kwa nini wasifungwe, lakini msajili hakuwapa nafasi ya kuwasikiliza wala kuhoji kwa sababu jalada mama la kesi hiyo liko Mahakama ya Rufaa.

Katika kiapo kilichoapwa na Mwalusaka, anadai kwamba msuluhishi wakati akitoa uamuzi hakutilia maanani nafasi ya Yanga, kwani haina mali za kuiwezesha kulipa fedha hizo, hivyo wanaomba uamuzi ubatilishwe.

Habari hii ni kwa hisani ya Mtanzania.

No comments:

Post a Comment

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...