Tuesday, April 15, 2014

Mke wa Rais wa Kenya aweka historia London, akimbia mbio za Marathon.


Mama Margaret Kenyatta mke wa Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta, amekuwa mwanamke wa kwanza mama wa taifa kushiriki mbio za London Marathon na kumaliza mbio hizo.
Alishangiliwa na wakenya wanaoishi nchini Uingereza alipomaliza mbio hizo za kilomita 42 kwa muda wa saa saba na dakika nne siku ya Jumapili.
Bi Kenyatta akilakiwa na mumewe Rais Uhuru Kenyatta

Bi Kenyatta alishiriki mbio za London Marathon kama sehemu ya mradi wake wa kuchangisha pesa za kuwasaidia wanawake wajawazito kujifungua katika mazingira salama na kuhakikisha kuwa watoto wao pia wanaishi nchini Kenya.Mama Margaret alilakiwa na Rais Kenyatta pamoja na waandalizi wa mbio hizo mjini London mwishoni mwa mbio huku akiwapa motisha wakenya na jamii ya kimataifa kwa kuwa mke wa kwanza wa rais kuwahi kushiriki mbio hizo.
Lengo lake kuu ni kupunguza idadi ya vifo vya wanawake wajawazito na watoto wachanga.
Wanawake wengi na watoto wachanga nchini Kenya hupoteza maisha yao wakati wa kujifungua kutokana na ukosefu wa huduma salama na sasa mama Kenyatta amejitwika jukumu la kuwapa akina mama wajawazito uwezo wa kujifungua salama.
Bi Kenyatta alikuwa na kikundi cha wasaidizi 8 waliokuwa naye hadi alipofika mwishoni mwa mbio hizo.
Wakenya kutoka sehemu mbali mbali uingereza walifika mjini London kushuhudia Bi Kenyatta akikamilisha mbio hizo.
Wakenya ndio walioshinda mbio hizo upande wa wanawake na wanaume.
Wilson Kipsang aling'aa upande wa wanaume kwa kuweka rekodi mpya ya saa mbili na dakika nne. Kipsang alifuatiwa na mkenya mwenzake Stanley Biwott.
Kwa upande wa wanawake, Edna Kiplagat alishikilia nafasi ya kwanza akifuatiwa na mkenya mwenzake Florence Kiplagat

Chanzo : BBC

No comments:

Post a Comment

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...