Thursday, April 11, 2013

AZAM MWENDO MDUNDO,YAWANYUKA AFRICAN LION 3-1


Ligi kuu ya Vodacom imeendelea tena leo kwa mechi moja katika uwanja wa Azam Complex kati ya Azam na african Lion na mpaka dakika 90 zinakamilika Azam 3- Af. Lion 1.
Azam anazidi kumsogelea kinala wa ligi Yanga.

KUNDI LA BOKO HARAM LAKATAA MSAMAHA NIGERIA



Kundi la wapiganaji wa kiisilamu nchini Nigeria, Boko Haram , limekataa pendekezo la kukubali msamaha.
Wiki jana Rais Goodluck Jonathan, aliuomba mkutano wa maafisa wakuu wa usalama kutafakari swala la kuwapa msamaha wapiganaji hao ili kuwashawishi kusitisha harakati zao.
Tangazo na mtu anayeaminika kuwa kiongozi wa kundi hilo Abubakar Shekau.
Katika miaka ya hivi karibuni, Boko Haram imekuwa ikiendesha kampeini ya ghasia na vurugu katika eneo la Kaskazini mwa nchi, na kuwaua takriban watu 2,000.
Kundi hilo linasema kuwa wapiganaji wake wanapigania kile wanachosema ni taifa la kiisilamu katika eneo la Kaskazini ambalo lina idadi kubwa ya waisilamu.
Bwana Shekau alisema kuwa kundi lake halijakosa hata kidogo, na kwa hivyo msamaha kwao sio jambo la kuzungumzia.
Aidha Shekau aliongeza kuwa ni jeshi la Nigeria ambalo linakiuka haki za waisilamu.
"nashangazwa kwa kuwa serikali ya Nigeria inazungumzia kuhusu msahama. Sisi tumefanya makosa gani? Ni sisi ambao tunapaswa kuwasamehe.'' alinukuliwa akisema Shekau
Mwandishi wa BBC nchini Nigeria,Will Ross, anasema kuwa viongozi wa kisiasa na kidini Kaskazini mwa nchi, wamekuwa wakimtaka rais Jonathan kuwasamehe wapiganaji hao, wakisema kuwa hatua za kijeshi dhidi ya wapiganaji hao hazisaidii kuleta amani.
Jopo la kutoa msahama liliundwa na serikali wiki jana na linajumuisha waakilishi wa jeshi.

Habari hii kwa hisani ya BBC

KUKITHILI KWA UCHAFU SOKO LA JIJI LA ARUSHA

Soko Kuu la jijini Arusha, limekithiri kwa takataka zinazotoa harufu mbaya  ambayo inalalamikiwa na baadhi ya wafanyabiashara kuwa inahatarisha usalama wa afya zao.

Wafanyabiashara hao wakiwemo wanaomiliki maduka yanayolizunguka soko hilo, waliliambia gazeti hili kwamba takataka hizo zinatupwa nje ya soko.

Hata hivyo walalamikaji hao hawakutaka majina yao yatajwe lakini walisema takataka  hizo zimerundikwa kwa  muda mrefu  bila ya kuzolewa na mamlaka zinazohusika.
Wafanyabiashara hao walisema katika kipindi hiki ambacho mvua zimekuwa zikinyesha mfululizo mkoani humo,  wamekuwa wakizishuhudia taka hizo zikioza na hatimaye kutoa harufu mbaya.
Mkuu wa soko hilo, John Lugiza alikiri kuhusu kuwapo kwa taka hizo na kwamba ni  kero hata kwa uongozi wa soko hilo.

Alisema kutokuzolewa kwa takataka hizo kunasababishwa na  gari kushindwa kuingia ndani ya soko na kwamba dampo la Muriet nalo  limejaa maji.


Habari hii kwa hisani ya Mwananchi.

SAFARI YA TANZANIA NA KIPANYA

Kwa vikwazo hivi kweli tanzania tutafika?????? Tafakari,Chukua hatua.

MAWAZIRI SASA HAWARUHUSIWI KUTOA SHUKRANI NA POLE BUNGENI

Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kanuni za Bunge na Naibu Spika, Job Ndugai
KUANZIA sasa Bunge limepitisha kanuni za kuwabana mawaziri kutoa salamu za pongezi, shukrani na pole pindi wanapokuwa wakizungumza bungeni. Pia Mawaziri hao wamezuiwa kutaja majina ya wabunge waliochangia bajeti zao kwa kuwa kufanya hivyo ni kutumia vibaya muda wa Bunge.
Kauli hiyo, ilitolewa bungeni jana na Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kanuni za Bunge ambaye pia ni Naibu Spika, Job Ndugai, alipokuwa akiwasilisha Azimio la Marekebisho ya Kanuni za Bunge.

Pamoja na mambo mengine, Naibu Spika alitoa kauli hiyo alipokuwa akifafanua kauli ya Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu (CHADEMA), aliyeonyesha kutoridhishwa na jinsi Spika wa Bunge anavyotumia Kanuni za Bunge juu ya matumizi ya muda.

Katika mazungumzo yake alipokuwa akichangia marekebisho ya kanuni hizo za Bunge, Lissu alimshutumu Spika wa Bunge, Anne Makinda, kwamba anachangia kwa wabunge na mawaziri kupoteza muda kwa sababu wanapokuwa wanazungumza bungeni, husema maneno ambayo hayana msingi wowote bungeni.

Kwa mujibu wa Lissu, kitendo cha mawaziri na wabunge kutoa pole, kutoa pongezi na kushukuru bungeni, ni maneno yasiyokuwa na maana na kwamba kitendo cha Spika kuyaruhusu kinakiuka Kanuni ya 154 ya Bunge.

“Mheshimiwa Spika, pamoja na kusema hayo, naomba niseme jambo hili na nalielekeza kwako moja kwa moja na hili linahusu matumizi ya muda.

“Kiti chako kina nguvu sana na baadhi yetu tunaona kama kiti chako kitatumia vizuri Kanuni za Bunge, tunaweza kuokoa muda mwingi unaopotea bila sababu.

“Huu utaratibu wa mheshimiwa kusimama na kutoa pole, kutoa pongezi unapoteza muda bure na unakiuka kanuni za Bunge. Kwa hiyo, naomba tuweke utaratibu ili ikiwezekana Spika ashukuru au apongeze kwa niaba ya Bunge na Waziri Mkuu apongeze kwa niaba ya Serikali.

“Naamini kama tukifanya hivyo, wabunge watapata muda wa kuchangia badala ya huu utaratibu wa sasa ambapo muda unapotea bila sababu,” alisema Lissu.

Akitoa ufafanuzi wa kauli hiyo, Naibu Spika aliungana na Lissu na kusema kuwa japokuwa siyo busara Spika kumkatisha mbunge asizungumze, wabunge na mawaziri wanatakiwa kutumia muda vizuri kwa kujielekeza kwenye hoja moja kwa moja.

“Marekebisho haya ninayowasilisha hapa, yanalenga kuitendea haki bajeti ya Serikali, kwani wabunge sasa wanapata muda wa kujadili bajeti za wizara kabla ya ile bajeti kuu.

“Kuhusu suala la muda wa kuchangia, marekebisho haya mapya yanasema mbunge atakuwa akichangia kwa dakika 10, wakati wa Bunge la Bajeti na atakuwa akitumia dakika 15 wakati wa Bunge la kawaida.

“Lakini, chama kinaweza kuomba zile dakika kumi zigawanywe kwa wabunge wawili ili kila mmoja achangie kwa dakika tano. Juu ya hili suala la wabunge na mawaziri kutoa pongezi, shukrani na kutoa pole na mawaziri kutaja majina ya waliochangia bajeti zao, kuanzia sasa halitaruhusiwa na nawashauri wabunge kila mnaposimama mwende kwenye hoja na kama unajijua huna hoja, tafadhali usisimame kuzungumza,” alisema Naibu Spika.

Awali katika mazungumzo yake, mbali na kutoridhishwa na jinsi muda unavyotumiwa bungeni, Lissu alilisisitiza Bunge, kwamba kilichokuwa kimewasilishwa na Naibu Spika kilihusu sehemu ya tisa ya Kanuni za Bunge, inayohusu masuala ya fedha na kwamba isije ikatafsiriwa kwamba marekebisho hayo yamegusa na maeneo mengine.

Kuhusu muda wa wabunge kuchangia, aliunga mkono kila mbunge atumie dakika kumi badala ya 15 zilizokuwa zikiruhusiwa kikanuni kwa kile alichosema kuwa, mabadiliko hayo yatawafanya wabunge wengi wazungumze.

Pamoja na hayo, alisema kuna haja Bunge kuangalia upya kanuni ya 96, kifungu cha pili, cha tatu na cha nne kinachompa waziri mamlaka ya kuweka ukomo wa bajeti yake.

Naye, Mbunge wa Viti Maalum, Anna Abdallah (CCM) na Mbunge wa Wawi, Hamad Rashid Mohamed (CUF), waliunga mkono kwa nyakati tofauti marekebisho hayo na kusema yanalenga kulipa nguvu Bunge. Pamoja na mjadala huo, Bunge lilipitisha marekebisho hayo.

Tuesday, April 2, 2013

UKOSEFU WA MAJI NA KIBONZO CHA MASOUD KIPANYA LEO

Hii ni habari iliyokatika mfumo wa kibonzo,lakini kutokana na hali halisi ilivyo huko mitaani maeneo mengi ya Tanzania kibonzo hiki kinaweza kuwa kweli.

RAIS KIKWETE AKUTANA NA NAIBU RAIS WA KENYA WILLIAM RUTO.

Rais kikwete akiongea na Naibu Rais Mteule wa Kenya Mh.William Ruto
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt Jakaya Mrisho Kikwete leo (jana) Aprili 1, 2013 amekutana na Naibu Rais mteule wa Kenya Mhe William Kipchirchir Samoei arap Ruto  ambaye alikuwa nchini kwa mapumziko ya Pasaka.
Akiongea na mgeni huyo katika hoteli ya Seronera iliyoko katika mbuga ya wanyama ya Serengeti  mkoani  Mara, Rais Kikwete  amempongeza Mhe Ruto na Rais mteule wa Kenya Mhe. Uhuru Kenyatta, kwa ushindi wao kwenye uchaguzi mkuu nchini Kenya.
Mhe Rais pia alimueleza Mhe Rutto furaha yake pamoja na kuridhishwa  na jinsi  uchaguzi ulivyofanyika kwa amani katika nchi hiyo.
Alielelezea  matumaini yake ya kuwa  urafiki uliopo kati ya Tanzania na Kenya  utadumishwa  pamoja na kusukuma mbele gurudumu la maendeleo ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Mhe Rutto, ambaye aliwasili Mkoani  Mara wiki  iliyopita akiwa na mke wake na watoto, ameondoka  leo baada ya chakula cha mchana alichoandaliwa na mwenyeji wake.

Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu.
Dar es Salaam.

AMUUA MKEWE BAADA YA KUMFUMANIA

 Antony Lutta - Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tabora
Mkazi mmoja wa Kijiji cha Idubula, katika Kata ya Karitu ,wilayani Nzega, Tabora, amemuua mkewe kwa kumkatakata kwa mapanga baada ya kumfumania.

Akiongelea tukio hilo Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Tabora, Antony Lutta, alisema tukio hilo lilitokea usiku wa mkesha wa Sikukuu ya Pasaka.

Lutta alisema mtuhumiwa alimfumania mke wake Veronica Maganga (20) akiwa chumbani kwake na mwanamume mwingine .

Kwa mujibu wa kamanda huyo, mwanamume huyo alifanikiwa kukimbia.
Alisema  hasira za mtuhumiwa katika tukio hilo  ziliishia kwa kumtakata mke kwa panga hadi alipokufa.

Kamanda Lutta aliwataka wananchi kutojichukulia sheria mikononi mwao na badala yake, waviachie vyombo vya dola kuchukua hatua dhidi ya watuhumiwa.
“Watu wamekuwa na tabia ya kujichukulia sheria mikononi kwa kuwahukumu watuhumiwa, huo ni ukiukwaji mkubwa wa sheria za nchi na tunawasihi waache,” alisema kamanda huyo.

Alisema mtuhumiwa wa tukio hilo atafikishwa mahakamani mara baada ya kukamilika kwa upelelezi.

Habari hii ni kwa hisani ya Mwananchi.

RUFAA YA SERIKALI DHIDI YA ZOMBE KUANZA KUSIKIRIZWA APRILI 22.


Abdallah Zombwe akihamaki
RUFAA ya kupinga kuachiwa huru kwa aliyekuwa Mkuu wa Upelelezi wa Mkoa wa Dar es Salaam, Abdallah Zombe na wenzake, inatarajiwa kusikilizwa mfululizo kuanzia Aprili 22 na 23 mwaka huu.

Rufaa hiyo imepangwa kusikilizwa mbele ya jopo la majaji watatu wa Mahakama ya Rufani ambao ni Jaji, Edward Rutakangwa, Jaji Mbarouk Mbarouk na Jaji Bernard Luanda.

Mbali na Zombe, wajibu rufani wengine ni polisi Christopher Bageni, Ahmed Makele, Jane Andrew, Koplo Emmanuel Mabula, Michael Shonza, Abeneth Saro, Rajabu Bakari na Festus Gwasab.

Serikali ilikata rufani hiyo kupinga hukumu iliyotolewa Agosti 17, mwaka 2008 na Jaji Salum Massati wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam.

Jaji Massati katika hukumu hiyo aliwaachia huru Zombe na wenzake waliokuwa wakikabiliwa na kesi ya mauaji ya wafanyabiashara watatu wa madini wa mkoani Morogoro na dereva teksi.

Zombe na wenzake walikuwa wakidaiwa kuwa Januari 14, mwaka 2006 waliwaua wafanyabiashara watatu wa madini wa wilayani Ulanga mkoani Morogoro; Ephraim Chigumbi, Sabinus Chigumbi na Mathias Lukombe na dereva teksi, Juma Ndugu, mkazi wa Dar es Salaam.

Katika hukumu hiyo, Jaji Massati alisema upande wa mashitaka ulishindwa kuthibitisha mashitaka bila ya kuacha shaka yoyote na hivyo mahakama iliwaona washitakiwa hawakuwa na hatia na kuwaachia huru.

Alisema mahakama hiyo ilibaini wauaji halisi walikuwa hawajafikishwa mahakamani na hivyo mashitaka dhidi ya washitakwa yasingeweza kutengenezeka. Aliuagiza upande wa Jamhuri iwasake na kuwafikisha mahakamani wahusika.

Baada ya kutolewa kwa hukumu hiyo, Mkurugenzi wa Mashitaka wa Serikali (DPP) aliamua kukata rufaa Mahakama ya Rufani, iliyosajiliwa na kupewa namba 254/2009 kupinga hukumu hiyo akidai hakuridhika nayo.
Katika rufani hiyo, DPP aliwasilisha hoja 11 za sheria kupinga hukumu hiyo akidai kwamba kwa mujibu wa ushahidi uliotolewa mahakamani, washitakiwa wote walikuwa na hatia.

Miongoni mwa sababu nyingine, DPP anadai kulikuwa na upungufu katika hukumu hiyo kwa kila mshtakiwa.

Anadai Jaji Massati alipotoka na kushindwa kutafsiri sheria na kanuni mbalimbali zinazohusu mashitaka ya jinai na kwamba alijichanganya katika hukumu hiyo.

DPP anadai kushangazwa na Jaji Massati kushindwa kuwatia hatia washitakiwa wote ikizingatiwa ulikuwapo ushahidi wa dhahiri na wa mazingira wa kutosha kuwatia hatiani.

Habari hii ni kwa hisani ya Mtanzania.

MAAFA, KIFUSI CHAUWA, 20 WAHOFIWA KUFA HUKO ARUSHA

Wakazi wa Arusha wakiwa eneo ambapo watu zaidi ya 20 wanahofiwa kufukiwa.
Siku tatu baada ya ghorofa kuanguka na kuua watu 36 jijini Dar es Salaam, maafa mengine yametokea jana mkoani Arusha ambako watu wapatao 20 wanahofiwa kufa baada ya kufunikwa na kifusi cha `moramu’ wakati wakifanya shughuli za uchimbaji eneo la Moshono, Arusha.

Maiti za watu 14 ndiyo zilikuwa zimeopoelewa hadi jana jioni wakati watu wawili tu ndiyo walikuwa wametoka wakiwa hai na kukimbizwa katika Hospitali ya Mt Meru kwa ajili ya matibabu kutokana na kuvunjika miguu.

Waliotolewa wakiwa hai walitambuliwa kuwa ni Matei Nenano na Lushooki Laizer wote wakazi wa jijini Arusha. Mwananchi lilishuhudia vikosi vya uokoaji kutoka Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), Polisi pamoja na wananchi wakitoa msaada wa kufukua kifusi hicho kwa ajili ya kutoa watu waliofunikwa.

Maiti zilizoopolewa ni za mmiliki wa magari ya kubeba kifusi hicho, Julius Peter, Alex Mariaki, Gerald Lutakata, Hassan Hamis, Sauli Raphael, Bariki Revelian na Kababuu Ruafela.
Wengine ni Mwenda Kiboliboli, Japhet Jivaline, Benard Masai, Gerald Jacob, Fredy Losileani, Julius Palangyo na mtu ambaye alijulikana kwa jina moja la Christopher.

Watu walioshuhudia tukio na taarifa hizo kuthibitishwa na Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Hemed Kilonge walisema lilitokea jana saa 5.00 asubuhi wakati shughuli za uchimbaji zikiendelea.

Kamanda Kilonge alisema wakati wachimbaji hao wakiwa ndani ya shimo wakiendelea na kuchimba ‘moramu’, ghafla gema liliporomoka na kuwafunika.

Mashuhuda walisema wachimbaji hao walikuwa wakifanya shughuli zao huku mvua kubwa ikinyesha na kwamba kuna uwezekano hiyo ni sababu ya kuanguka kwa kifusi hicho.
Mvua ilikuwa ikiendelea hata wakati wa uokoaji, hali iliyofanya kazi hiyo kuwa ngumu.

“Inasadikiwa kuwa zaidi ya wachimbaji 20 pamoja na magari mawili kwa ajili ya kubeba mzigo huo yalikuwapo ndani ya shimo hilo ambayo nayo yalifunikwa na kifusi hicho,”alisimulia Kamanda Kilonge.

Uhaba wa mafuta
Mwananchi lilishuhudia magari ya uokoaji kutoka jijini Arusha yakiwa yameishiwa mafuta na kusababisha uokoaji kuzorota.

Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Magesa Mulongo amelazimika kusitisha safari yake mkoani Tanga baada ya kupata taarifa ya tukio hilo na baadaye alitangaza kwamba Serikali imeamua kufunga machimbo yote ya `moramu’ hadi pale itakapotoa tamko lingine.

Akizungumza eneo la tukio, Mulongo alisema tukio hilo ni la kusikitisha kwa kuwa vijana waliokufa ni wengi.
Kwa upande wake mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema aliitaka Serikali kuweka utaratibu wa kukabiliana na matukio ya aina hiyo ikiwa ni pamoja na kuweka viashiria vya usalama maeneo ya machimbo.
Godbles lema Mbunge wa Arusha Mjini
Kiongozi mwingine aliyefika katika eneo hilo ni Meya wa Jiji la Arusha, Gaudence Lyimo ambaye alisema kwa sasa ni muda mwafaka wa kufunga mgodi huo kwa kuwa mwaka 1997 tukio kama hilo lilitokea na kuua watu saba kwa kufukiwa na kifusi.
Joshua Nasari Mbunge wa Arumeru Mashariki.
Mbunge wa Arumeru Mashariki, Joshua Nasari aliilalamikia Serikali kwa kutokuwa na ofisi ndogo za vitengo vya maafa mikoani na kudai kuwa endapo ofisi hizo zingekuwapo uokoaji ungekuwa rahisi.

Wananchi wafurika
Wananchi kutoka viunga mbalimbali vya Jiji la Arusha walijitokeza kwa wingi kushuhudia kazi za uokoaji zikiendelea bila kujali mvua kubwa iliyokuwa ikinyesha.
Wananchi hao walionekana kushirikiana katika uokoaji ambapo ilipofika saa 10.00 jioni, wanajeshi zaidi kutoka Kambi ya 977KJ na Sopa Monduli walifika kuongeza nguvu.
 Wakizungumzia tukio hilo, baadhi ya wananchi waliitupia lawama Serikali kwa kushindwa kuweka usimamizi mzuri wa machimbo hayo licha ya tukio kama hilo kuwahi kutokea siku za nyuma.

“Hii ni mara ya pili kwa machimbo haya kusababisha vifo. Mwaka 1997 tulishuhudia machimbo haya yakiporomoka na watu kufunikwa ndani lakini hakuna hatua iliyochukuliwa mpaka leo tunashuhudia haya tena. Ni lazima Serikali iwajibike kutokana na mauaji haya,”alisema mzee aliyejitambulisha kwa jina la Christoper Laizer.

Habari hii ni kwa hisani ya Mwananchi

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...