Tuesday, March 18, 2014

WIKI YA MAJI YAFANA MOROGORO.

Mgeni Rasmi Mstahiki Meya wa Manispaa ya Morogoro Mh.Amir Nondo 
Kila mwaka Wizara ya maji huadhimisha wiki ya maji nchini kote kuanzia tarehe 16-22, Machi. Katika kipindi hiki cha maadhimisho haya Mamlaka za maji nchini hufanya kazi mbali mbali ikiwa ni pamoja na kufanya mikutano na wadau wa maji,kusafisha mazingira, kuhamasisha wananchi katika kulinda na kutunza vyanzo vya maji, maadhimisho haya pia hulenga katika kuwaelimisha wananchi kuhusu sera ya taifa ya maji na mikakati yake ya utekelezaji.
Mkurugenzi mtendaji wa MORUWASA akimueleza Mh.Meya jinsi ya mto Mlali ulivyovamiwa na kuendelea kulima mdani ya mto.
CHIMBUKO LA MAADHIMISHO
Kwa kipindi cha miaka 25 sasa Tanzania imekuwa ikiadhimisha Wiki ya Maji kila mwaka. Chimbuko la Maadhimisho ya Wiki ya Maji Kitaifa ni Azimio la Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Wahandisi wa Maji uliofanyika Mkoani Shinyanga Mwaka 1987. Aidha, mwaka 1992 Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa ulipitisha Azimio Na. 47/193 kuwa tarehe 22 Machi ya kila mwaka, nchi wanachama waadhimishe Siku ya Maji Duniani, ambayo ni Kilele cha Wiki ya Maji.
Msitahiki Meya wa manispaa ya Morogoro akiongea na wakazi wa Mlali pamoja na watumishi wa MORUWASA na Bonde la Wami/Ruvu.
KAULIMBIU YA MAADHIMISHO
Maadhimisho haya huwa na kaulimbiu tofauti mwaka hadi mwaka. Kaulimbiu ya Wiki ya Maji kwa mwaka huu ni “Uhakika wa Maji na Nishati”. Kaulimbiu hii imetokana na kaulimbiu ya Siku ya Maji Duniani ambayo ni  “Water and Energy”. Ujumbe huu unaweka mkazo ili kuona umuhimu wa Maji na Nishati kwa pamoja. Maji na Nishati ni rasilimali zenye umuhimu sana kwa maisha ya binadamu, huduma za Maji na Nishati zinategemeana sana, kutokana na uhusiano uliopo kati ya rasilimali maji na uzalishaji wa nishati, kwa upande mmoja maji yanategemea nishati ili yasafirishwe kwenda maeneo mbalimbali katika mfumo kuanzia kwenye chanzo, kupitia mitambo ya kusukuma na kusafirisha hadi hapo yanapomfikia mtumiaji. Katika upande mwingine upatikanaji wa Nishati unategemea kuwapo kwa maji ya uhakika katika uzalishaji.
Ili kwenda sambamba na kaulimbiu katika kuadhimisha wiki ya maji , MORUWASA imeamua kwa kushirikiana na Ofisi ya Bonde la Wami/Ruvu kuweka mipaka katika vyanzo vya maji hasa mito inayoingiza maji katika bwawa la Mindu kwa kupanda Mikatani kuanzia kwenye chanzo cha mito hiyo huko milimani hadi bwawa la Mindu.
Aidha, MORUWASA itatembelea wateja wake katika Manispaa ya Morogoro ili kuwahamasisha na kuwaelimisha kuhusu Hali halisi ya upatikanaji wa huduma ya majisafi katika maeneo yao na majitaka kwa ujumla.
Wananchi wa Mlali waliokutwa wakifua nguo katika mto Mlali.
UMUHIMU WA UTUNZAJI WA MAZINGIRA KATIKA VYANZO VYA MAJI

Kama tunavyofahamu kuwa MAJI NI UHAI, ni jambo la muhimu kusisitiza utunzaji wa vyanzo vya maji ili kuifanya huduma ya maji kuwa endelevu. MORUWASA inawaomba na kuwashauri wananchi wote kuachana na vitendo vya kuharibu mazingira kwa kuchoma moto, kulima kwenye miteremko mikali bila ya kuzingatia utaalam wa kilimo cha miinuko na kuacha kabisa uchimbaji wa dhahabu na kokoto kandokando ya mito.

No comments:

Post a Comment

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...