Thursday, February 13, 2020

MKUTANO WA KWANZA WA KAMATI YA MAWAZIRI WENYE DHAMANA YA MENEJIMENTI YA MAAFA KWA NCHI WANACHAMA WA JUMUIYA YA MAENDELEO KUSINI MWA AFRIKA

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Kazi , Ajira,  Vijana na Watu wenye Ulemavu), Mhe. Jenista Mhagama akiongea na Waandishi wa Habari kuhusu Mkutano wa Kwanza wa Kamati ya Mawaziri wenye dhamana ya Menejimenti ya Maafa kwa Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika utakaofanyika tarehe 18 – 21 Februari, 2020, Zanzibar. Mgeni Rasmi, atakayefungua mkutano huo ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi.Mhe Dk. Ally Mohamed Shein.
Ndugu Wananchi,
Serikali ya Tanzania itakuwa mwenyeji wa Mkutano wa Kwanza wa Kamati ya Mawaziri wenye dhamana ya Menejimenti ya Maafa kwa Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika utakaofanyika tarehe 18 – 21 Februari, 2020, Zanzibar. Mgeni Rasmi, atakayefungua mkutano huo ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi.Mhe Dk. Ally Mohamed Shein.
Kaulimbiu ya Mkutano huu: “Ushiriki wa Kisekta kwenye Kupunguza madhara ya maafa ni njia bora ya kuimarisha ustahimilivu katika ukanda wan chi Wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika” (SADC).
Itakumbukwa kuwa Tanzania ilichukua rasmi nafasi ya Mwenyekiti wa jumuiya kuanzia mwezi Agosti, 2019 kwa kipindi cha mwaka mmoja hadi mwezi Agosti, 2020.  Hatua hii inatokana na utaratibu wa kawaida wa mzunguko wa kushika nafasi hiyo kulingana na mkataba wa kuanzishwa kwa jumuiya hiyo.
Mkutano huu unafanyika kwa mara ya kwanza visiwani Zanzibar tangu Mhe. Dkt. John Joseph Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akabidhiwe uenyekiti wa jumuiya. Kufanyika kwa mkutano huu ni fursa kubwa kwa wananchi wa Tanzania kwani utasaidia kukuza biashara na utalii katika nchi yetu hasa visiwa vya Zanzibar na kuendelea kujitangaza kimataifa.

Ndugu Wananchi,
Kamati ya Mawaziri wenye dhamana ya menejimenti ya Maafa  imeanzishwa kwa lengo la kulishauri Baraza la Mawaziri wa nchi za jumuiya ya SADC kuhusu masuala ya upunguzaji wa madhara ya maafa kikanda. Lengo mahususi pia ni,  kuwa jukwaa la kubadilishana taarifa na uzoefu wa kiutendaji miongoni mwa nchi wanachama ili kutekeleza kwa ufanisi shughuli za usimamizi wa maafa.
Ndugu Wananchi,
Mkutano huu unakuja kipindi ambacho nchi nyingi wanachama katika ukanda huu zimekuwa zikiathiriwa na majanga ya asili mara kwa mara na kusababisha madhara makubwa. Sote tunakumbuka ukame wa mwaka 2016 ambao uliathiri takribani watu milioni 40 katika ukanda huu na kusababisha ukosefu wa chakula. Idadi hii iliongezeka hadi watu milioni 41.6 katika nchi 13 Wanachama kipindi cha msimu wa 2018/2019.
Ndugu Wananchi,
Baadhi ya nchi wanachama ikiwemo; (Komoro, Malawi, Msumbiji na Zimbabwe) kwa mwaka 2019 zilipata mafuriko yaliyosababishwa na Vimbunga Idai na Kenneth. Kutokana madhara ya mafuriko hayo, Gharama za misaada kukabilia na madhara zilikadiriwa kuwa dola milioni 323, wakati gharama za kurejesha hali zilikadiriwa kuwa dola bilioni 10.
Ili kuweza kupunguza gharama kubwa katika urejesahi wa hali ndio maana katika mkutano wa SADC kujadiliana namna ya kuwekeza katika punguza madhara ya maafa, kwa kuwa Gharama za usimamizi wa maafa kama ya ukamae na mafuriko huzilazimu Nchi Wanachama kuelekeza rasilimali zilizotengwa kwa ajili ya shughuli za za maendeleo na badala yake kuelekezwa katika shughuli kurejesha hali.
Sote tunakumbuka, matukio ya Vimbunga vya Idai na Keneth, katika nchi za Msumbiji, Malawi na Zimbabwe,  zilizoathirika zaidi. Kutokana na madhara ya Vimbunga  hivyo,  Nchi yetu ilishiriki katika hatua za kurejesha hali,  kwa kutoa misaada ya kibinadamu: ikiwemo tani 24  za dawa za binadamu na mahindi tani 200 kwa nchi  hizi 3 (Msumbiji, Malawi na Zimbabwe).
Ndugu Wananchi,
Kwa uzoefu wa aina ya majanga ambayo hutokea katika nchi za SADC, yanadhihirisha umuhimu wa ushirikiano wa kikanda ulio thabiti katika kukabiliana nayo. Majanga haya kwa kiasi kikubwa yanatokana na mabadiliko ya tabianchi na hali ya hewa, Pia yamekuwa yakitokea magonjwa ya milipuko ya wanyama na mazao, katika ukanda huu ambao asilimia kubwa ya wananchi wake hutegemea sana shughuli za kilimo kwa ustawi wa uchumi.

Hali hii imekuwa ikichangia kudumaza ukuaji wa uchumi wa kikanda, hivyo hatuna budi kuchukua hatua kwa pamoja za kupunguza madhara, kuimarisha utayari wa kikanda na uwezo wa kukabiliana na maafa.
Aidha, katika kuchukua hatua za kuimarisha ustahimilivu wa kikanda dhidi ya maafa, Sekretarieti ya Jumuiya kwa kushirikiana na nchi wanachama imekuwa ikifanya juhudi mbalimbali za kuimarisha ustahimilivu kwa kuandaa Mpango wa Dharura wa Kujiandaa na Kukabiliana na Maafa,  kushirikiana kuandaa taarifa za utabiri wa msimu na kutoa tahadhari ya awali kuhusu hatari zitokanazo hali ya hewa pamoja na kutoa mafunzo kwa wataalam wa nchi wanachama katika fani mbalimbali ikiwemo tathmini, utafutaji na uokoaji.
Aidha, baadhi ya nchi wanachama ikiwemo Tanzania zimefaidika kwa kupata vifaa na mifumo ya kufuatilia majanga ya mafuriko, ukame na moto wa misituni kwa ajili ya kutoa tahadhari ya awali.
Ndugu Wananchi,
Ili kwenda sambamba na juhudi za kikanda na kimataifa, serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Dkt. John Pombe Magufuli,  itaendelea kuimarisha uwezo wake wa usimamizi wa maafa katika nyanja zote. Tayari serikali ya awamu ya Tano imetunga Sheria ya Usimamizi wa Maafa ya Kitaifa Na. 7 ya 2015 na kanuni zake, Tunao Wasifu wa Janga la Mafuriko na Ukame wa Kitaifa na Mkakati wa Taifa Kupunguza Madhara ya Maafa;
Serikali imefanikiwa kuandaa Mpango wa Dhamira ya Taifa wa Utekelezaji wa Makubaliano ya Paris kuhusu mabadiliko ya tabianchi, pia  Mfumo wa Taifa wa Ufuatiliaji na Taarifa za Gesi Joto umeandaliwa pamoja na  Mipango ya Kukabiliana na Dharura za afya ya binadamu, mifugo na wanyama pia na kuandaa Mkakati wa Taifa wa Usimamizi wa Mazao baada ya Kuvuna.
Lengo kubwa la serikali ni kuhakikisha kila sekta inazingatia hatua za upunguzaji wa madhara ya maafa katika mipango ya maendeleo na uandaaji wa bajeti ili kupunguza madhara kwa jamii na hasara za kiuchumi.
Ndugu Wananchi,
Mkutano wa Kwanza wa Kamati ya Mawaziri wanaohusika na Menejimenti ya Maafa kwa Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika utakaofanyika mwezi Februari, 2020 visiwani Zanzibar unakusudia kuchochea juhudi zilizopo katika kupunguza madhara ya maafa kwa kuteleleza yafuatayo:
       i.            Kujadili na kupitisha Mkakati wa Kujiandaa na Kukabiliana na Maafa wa Kikanda 2016 – 2030;
    ii.            Kujadili na kuridhia Mfumo Mkakati wa Ustahimilivu wa Kikanda 2020 – 2025;
  iii.            Kupitia maombi ya nchi wanachama kuunga mkono Sekretarieti ya Jumuiya kupata idhini ya matumizi ya Mfuko wa Fedha za Ufadhili wa Mabadiliko ya Tabianchi.
  iv.            Kupokea taarifa za maendeleo juu ya utekelezaji wa Mkakati wa Mabadiliko ya Tabianchi na Mpango Kazi;
     v.            Kupokea taarifa ya hatua za utekelezaji wa maazimio mbalimbali ikiwemo kuanzisha Mfuko wa Kujiandaa na Kukabiliana na Maafa wa Kikanda; kuanzisha Kituo cha Kikanda cha Operesheni ya Maafa; Mpango wa Mazoezi ya Nadharia ya Kukabiliana na Dharura; pendekezo la Mfumo wa Ushirikiano wa Rasilimali ikiwemo wataalam, fedha na vifaa wakati wa dharura; na Utafiti wa Njia Mbadala za Ufadhili wa Majanga katika huduma za kibinadamu na urejeshaji wa miundombinu kutokana na majanga ya asili.
Mhe. Jenista Mhagama (MB)
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu
Sera, Uratibu, Bunge, Uwekezaji, Ajira, Vijana na Wenye Walemavu

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Kazi , Ajira,  Vijana na Watu wenye Ulemavu), Mhe. Jenista Mhagama akiongea na Waandishi wa Habari kuhusu Mkutano wa Kwanza wa Kamati ya Mawaziri wenye dhamana ya Menejimenti ya Maafa kwa Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika utakaofanyika tarehe 18 – 21 Februari, 2020, Zanzibar. Kulia kwake ni, Mkurugenzi wa Menejimenti ya Maafa Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu, KanalI, Jimmy Matamwe.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Kazi , Ajira,  Vijana na Watu wenye Ulemavu), Mhe. Jenista Mhagama akiongea na Waandishi wa Habari kuhusu Mkutano wa Kwanza wa Kamati ya Mawaziri wenye dhamana ya Menejimenti ya Maafa kwa Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika utakaofanyika tarehe 18 – 21 Februari, 2020, Zanzibar. Mgeni Rasmi, atakayefungua mkutano huo ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi.Mhe Dk. Ally Mohamed Shein.

No comments:

Post a Comment

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...